Tanzania na Zambia wamekubaliana kubadilisha sheria ili kuruhusu mkurugenzi mkuu wa shirika la reli la TAZARA kupatikana kutoka nje ya nchi hizo mbili.
Uamuzi huo umetangazwa jijini Dar es Salaam ambapo Rais wa Zambia Edgar Lungu amefanya ziara ya kikazi ya siku tatu.

Taarifa ya pamoja imesema kuwa viongozi wa mataifa hayo mawili wanashawishika kwamba mabadiliko hayo ya kisheria yataliokoa shirika hili la reli kutoka hali ya maututi inayolikabili hivi sasa.
Sheria zinazoliongoza shirika hilo zinasema kwamba Mkurugenzi Mkuu wa shirika anapaswa kutoka Zambia huku makamu wake akitoka Tanzania.
Tazara imeshuhudia kuporomoka katika uwezo wa kuendesha shughuli zake ambapo kwa mujibu wa Rais John Magufuli, mwaka 1976 wakati wa uanzishwaji wake lilikuwa na uwezo wa kubeba mizigo ya tani milioni 5 kwa mwaka wakati hivi sasa lina uwezo wa kubeba tani Laki moja na elfu 28 tu.
Rais wa Zambia amesema kuwa shirika hilo linapaswa kuendeshwa kibiashara zaidi,ili liweze kurudisha faida ya uwekezaji ambao watu wa Zambia na China walifanya.
''Kinachotokea hivi sasa ni kwamba tunafungwa na matakwa ya kisheria kwamba uongozi wa juu wa shirika uundwe kwa mujibu wa sheria zilizopo.Lakini tumedhamiria sasa kwamba tunataka shirika hilo liendeshwe kibiashara zaidi, ili lirudishe faida ya uwekezaji ambao watu wa Zambia na China waliufanya''.
Mbali na kuporomoka kwa idadi ya mizigo inayosafirishwa na TAZARA, miaka ya hivi karibuni shirika hilo limezongwa na mlolongo wa migomo ya wafanyakazi waliokuwa wakidai malimbikizo ya malipo yao
Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli amesema: "Ukizungumza na uongozi wa TAZARA kwa vyovyote vile watakwambia kwamba wanahitaji mtaji, lakini ukweli tatizo ni uongozi. Kwasababu kama ni mtaji, walikuwa nao mwaka 1976, lakini huo mtaji umeshuka hata sasa hauonekani kama ni mataji tena"
Mambo mengine ambayo Rais Magufuli na mwenzake Rais Lungu waliyajadili ni pamoja na kupunguzwa kwa vizuizi vya barabarani katika usafirishaji wa mizigo lakini pia upanuzi au uboreshaji wa usafirishaji wa mafuta na gesi kutoka Tanzania kwenda Zambia kupitia bomba la mafuta la TAZAMA