Mwenyekiti wa Madereva Kanda ya ziwa Hassan Dede akihojiwa na waandishi wa habari



Askari wa kikosi cha usalama barabarani wakiwa
wamezisimamisha Daladala kwa kosa la kupakia abira eneo ambalo sio rasmi






 Jinsi magari yanavyogeuza katika eneo la Buhongwa
 Eneo la stendi isiyokuwa rasmi ya Buhongwa ilivyo katika kadhia ya ubovu
 Mwenyekiti wa Madereva Kanda ya ziwa Hassan Dede akikagua eneo la barabara ya Buhongwa ambayo inatumiwa na madereva Daladala kama stendi
 Gari likigeuza katikati ya barabara kutokana na kukosekana kwa eneo maalumu la stendi




 Wajasiriamali wakiwa katika eneo la biashara huku Daladala zikitumia eneo hilo pia kupakia na kushusha abiria
 Gari inageuza kituoni ambapo ni barabarani huku watu wakiendelea kuvuka barabara
 Dede akikagua barabara iliyoharibika
 Gari ikiwa imepaki katika eneo bovu la barabara ya Buhongwa






 Mwandishi wa habari wa www.wazo-huru.blogspot.com Mathias Canal akimhoji moja ya madereva katika eneo la Buhongwa


 Mwenyekiti wa madereva Kanda ya ziwa
Bw Hassan Dede akisalimia na wakazi wa eneo la Nyashishi mara baada ya kuzuru katika eneo hilo ambalo ndilo amependekeza kuwa stendi ya daladala, kushoto kwake ni Mwandishi wa habari wa www.blogspot.com Ndg Mathias Canal

Na Mathias Canal,
Mwanza

Uongozi wa Mkoa wa Mwanza umetakiwa kubainisha stendi za
Daladala, maeneo maalumu kwa ajili ya kufanyia biashara za mbogamboga na
matunda kwa kina mama sambamba na kubainisha maeneo maalumu ambayo daladala
haziruhusiwi kusimama kwani kufanya hivyo kutaondoa urasimu uliopo baina ya
madereva wa Daladala na askari wa usalama barabarani.

Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa madereva Kanda ya ziwa
Bw Hassan Dede wakati alipozuru kujionea kadhia wanazokumbana nazo madereva
wawapo barabarani sambamba na kujionea kandia wanayoipata kutokana na ubovu wa
barabara na kutokuwa na stendi ya Daladala katika Mtaa wa Buhongwa nje kidogo
ya Halmashauri ya Manispaa ya Nyamagana.

Dede alisema kuwa ni ajabu kwa nchi yetu kuwa na kituo cha
daladala chenye mwanzo lakini hakina mwisho hivyo kuwafanya madereva kugeuza
mahala pasipokuwa rasmi ambapo ni hatari kwa uhai na magari na madereva hao.

Katika eneo la Buhongwa zinapogeuzia daladala kama kituo,
barabara yake ni mbovu huku pembeni kukiwa na machinga sambamba na
wajasiriamali wanaouza mbogamboga na matunda jambo ambalo linaweza kusababisha
hatari kwa wafanyabiashara hao endapo kama gari litaharibika kutokana na
hitilafu ya breki.

Hata hivyo alisema kuwa kumekuwa na wimbi la ukamataji na
kutozwa faini na askari wa usalama barabarani kwa madereva hao kutokana na
kuegesha magari katika eneo la barabara kwa ajili ya kupakia abiria jambo
ambalo ni kinyume na utaratibu kwani hakuna kituo katika eneo hilo pamoja na
madereva hao kulipia ushuru kila siku.

Dede alisema kuwa katika njia itokayo Kishiri, Airport,
Ilemela na Kisesa kuelekea Buhongwa kuna jumla ya Daladala 1900 ambayo kwa siku
moja kila gari inalipia ushuru wa shilingi 1000 ambapo kwa gari zote 1900 kwa
siku serikali inakusanya kodi ya jumla ya shilingi 1,900,000/=.

Katika kipindi cha mwezi mmoja serikali inakusanya jumla ya
shilingi 57,000,000/= huku ikiwa inakusanya jumla ya shilingi 693,500,000 kwa
mwaka.

Dede amehoji fedha zote hizo serikali inafanyia nini kama
imeshindwa kukarabati barabara itokayo Mwanza Mjini kuelekea Airport sambamba
na kukarabati na kubainisha eneo maalumu la stedi kwa ajili ya Daladala.

Sambamba na hayo pia Dede amependekeza serikali kuhamisha
kituo cha daladala kisichokuwa rasmi cha Buhongwa kuhamia katika eneo la
Nyashishi lililopo mwanzoni mwa Wilaya ya Misungwi kwani kupitia kuwepo kwa
eneo hilo daladala zote zitafanikiwa kuingia katika stendi hiyo na serikali itakusanya
mapato mengi kwani itakuwa rahisi kuwabana madereva wote.

Katika Barabara itokayo Makao makuu ya Mkoa wa Mwanza (Ofisi
ya Mkuu wa Mkoa) kuelekea eneo hilo la Buhongwa kuna vituo rasmi visivyopungua
sita huku vituo visivyo rasmi vipo zaidi ya 15 hivyo ni vyema uongozi wa Mkoa
wa Mwanza kupitia ofisi ya usalama barabarani kusimamia jambo hilo na kuweka
alama mahususi zitakazobainisha vituo hivyo.

MWISHO