Klabu ya Chapecoense kutoka Brazil, ambayo iliwapoteza wachezaji 19 pamoja na wahudumu kwenye ajali ya ndege walipokuwa wakielekea kucheza fainali ya Copa Sudamericana, imetunukiwa kombe hilo.
Uamuzi huo umechukuliwa na shirikisho la soka la Amerika Kusini, Conmebol kufuatia ombi la wapinzani wa klabu hiyo.
Watu 71, wakiwemo wachezaji 19 na wahudumu wa klabu hiyo, walifariki Jumatatu wakielekea Colombia kwa mechi ya mkondo wa kwanza ya fainali ya kombe hilo.
Wapinzani wa klabu hiyo kutoka Atletico Nacional, ambao waliomba Chapecoense wapewe kombe hilo, wametunukiwa tuzo ya Uchezaji Haki ili kutambua "moyo wao wa amani, kuelewa na kucheza haki".
Chapecoense pia watapewa jumla ya $2m (£1.57m) ambazo hukabidhiwa mshindi.
Atletico Nacional nao watapewa $1m (£787,000).
Makamu wa rais wa Chapecoense Ivan Tozzo amesifu uamuzi huo na kuutaja kama "haki", akihutubia wanahabari Jumatatu.
"Tuna uhakika 'Chape' wangekuwa mabingwa. Ni heshima kubwa."
Wachezaji watatu wa Chapecoense ni miongoni mwa watu sita walionusurika ajali hiyo.
Uchunguzi kuhusu chanzo cha ajali hiyo unaendelea lakini sauti iliyonakiliwa na mitambo ya ndege hiyo inaashiria huenda ndege hiyo iliishiwa na mafuta kabla ya kuanguka karibu na mji wa Medellin.
Klabu kadha Brazil zimejitolea kuipa Chapecoense wachezajiImage copyrightDOUGLAS MAGNO
Image captionKlabu kadha Brazil zimejitolea kuipa Chapecoense wachezaji
Mji wa Chapeco nchini Brazil uliandaa ibada kubwa ya mazishi Jumamosi baada ya majeneza yenye miili ya waliofariki kufikishwa nyumbani yakiwa yamefungwa kwa bendera za klabu hiyo.
Watu 13,000 waliwasilisha maombi ya kutaka kuwa wanachama wa klabu hiyo katika kipindi cha siku mbili pekee.
Klabu za soka kote duniani, zikiwemo zile za Ligi ya Premia, zilitoa heshima kwa wachezaji waliofariki wakati wa mechi zilizochezwa wikendi.
Klabu zinazocheza Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya na ligi ndogo ya klabu, Europa League nazo zitakaa kimya dakika moja kabla ya mechi za wiki hii kutoa heshima kwa waliofariki.
Klabu kuu Brazil zimeahidi kuipa Chapecoense wachezaji kwa mkopo bila malipo yoyote na pia zimeomba klabu hiyo ipewe kinga na isishushwe daraja kwa misimu mitatu ijayo.
Chapecoense walitarajiwa kucheza mechi yao ya mwisho ligini msimu huu mnamo Jumapili 11 Desemba lakini mechi hiyo haitachezwa kwani haiathiri mshindi wa ligi wala anayeshushwa daraja.
Wachezaji wengi wa Chapecoense walifariki, pamoja na wanahabari 20 walioandamana naoImage copyrightAP
Image captionWachezaji wengi wa Chapecoense walifariki, pamoja na wanahabari 20 walioandamana nao
Kama washindi wa Sudamericana, Chapecoense wamehakikishiwa nafasi katika michuano ya Copa Libertadores, michuano mikuu ya klabu Amerika Kusini ambayo ni sawa na Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya.
Hii ina maana kwamba Chapecoense watakutana na Atletico Nacional, mabingwa watetezi wa Copa Libertadores, kwenye mechi mbili mwaka ujao, ambazo huchezwa kati ya mabingwa wa michuano hiyo miwili mikuu barani Amerika Kusini.
Mchezaji wa zamani wa Brazil na Barcelona Ronaldinho na nyota wa zamani wa Argentina Juan Roman Riquelme wanadaiwa kujitolea kuichezea klabu hiyo.
Mchezaji wa zamani wa Barca Eidur Gudjohnsen, pia yuko tayari kuchezea klabu hiyo.
Brazil watacheza dhidi ya Colombia mechi ya kirafiki mwishoni mwa Januari kuchangisha pesa za kusaidia waathiriwa wa ajali hiyo ya ndege.
Jeneza lenye mwili wa mmoja wa waliofariki likiingizwa kwenye uwanja wa michezo na wanajeshi wa BrazilImage copyrightGETTY IMAGES
Image captionJeneza lenye mwili wa mmoja wa waliofariki likiingizwa kwenye uwanja wa michezo na wanajeshi wa Brazil

Mada zinazohusiana