Maafisa wa usalama nchini Ghana wamewakamata watu watatu kwa kuhusishwa na kuwa na ubalozi bandia wa Marekani mjini Accra ambao umetumika kuwalaghai raia maelfu ya fedha kwa miaka 10.
Idadi kamili ya walaghai hao haijabainika, lakini walifumaniwa na polisi wa Ghana wakisaidiana na maafisa wa usalama wa ubalozi wa Marekani. Kwa sasa waliokamatwa wanahojiwa ili kuelezea zaidi kuhusu udanganyifu huo.

Genge linalosimamia ubalozi bandia liliwatafuta wateja kutoka mataifa jirani na ndani ya nchi kisha kuwaleta kwenye jengo lililokua na bendera ya Marekani. Kila mteja aliyekata kupata Visa ya kusafiri Marekani alitozwa dola 6,000. Baadhi ya Visa hata hivyo zilikua halisi, hali inayozua wasi wasi kwamba huenda walishirikiana na baadhi ya wafanyikazi wa ubalozi wa Marekani mjini Accra.
Waliokamatwa ni wenyeji na raia wa Uturuki.Wengi wa wateja waliodanganywa ni wakaazi wa maeneo ya mashambani, na waliamini ubalozi huo bandia baada ya kukutana na wanachama wa genge hilo kutoka Uturuki. Ubalozi huo bandia pia haukuwekwa kwenye mtandao na waliwapata wateja kwa kuzungumza na raia.