Rais Mteule wa Marekani, Donald Trump, ametangaza kuvunjilia mbali shirika lake la utoaji misaada, ili kuzuia aina yoyote ya muingiliano wa kikazi wakati akiwa Rais. Bwana Trump amesema shirika hilo limetoa msaada mkubwa wa mamilioni ya dola, ili kufadhili miradi mbalimbali, lakini sasa ameachana nalo kwa manufaa ya cheo chake mpya kama Rais wa Marekani. Mwanasheria mkuu wa New York, amekuwa akichunguza wakfu huo wa kibinafsi wa Bwana Trump, ikiwa unafuata kila kanuni ya sheria zinazolinda mashirika ya misaada na mchango kwa makundi mbalimbali ya kisiasa, na mwezi Oktoba mwaka huu, aliamuru ikome kukusanya fedha.