Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na mchambuzi wa masuala ya kisiasa na kijamii, Dk Benson Bana
WASOMI wamesema pamoja na mazungumzo ya Rais John Magufuli na mmiliki wa kiwanda cha Saruji cha Dangote kilichopo Mtwara, Aliko Dangote, kukata mzizi wa fitina, kauli thabiti ya serikali kukabiliana na wapiga dili waliokuwa wanakwamisha uendeshaji wa kiwanda hicho imeibua matumaini mapya kwa Watanzania.
Aidha makubaliano hayo yaliyofikiwa yatainua thamani ya shilingi kutokana na rasilimali za nchi kutumika kufanya mnyororo wa thamani unaojenga uchumi wa Watanzania.

Wasomi, wachambuzi wa masuala ya kisiasa na jamii, wafanyabiashara na wananchi wa kawaida wakiwemo wa Mtwara ambao ni sehemu ya wanufaika wa kiwanda hicho wamesema katika mahojiano na gazeti hili, kwamba wamefurahishwa na matokeo ya mazungumzo hayo.
Rais Magufuli alizungumza na Dangote baada ya uchafuzi wa hali ya hewa uliosababishwa na vyombo vya habari na wanasiasa na kuingiza hofu kubwa kwa wananchi ambao kwa asilimia kubwa walianza kunufaika na uwekezaji huo.
Akizungumza na gazeti hili jana, Mwanazuoni, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na mchambuzi wa masuala ya kisiasa na kijamii, Dk Benson Bana alimpongeza Rais kwa kufanya mazungumzo na Dangote kwani kupitia mazungumzo hayo yameweka sawa hali ya hewa.
Dk Bana alisema mazungumzo yaliyofanywa yamedhihirisha hatma ya Dangote, kwani utata uliokuwa umejitokeza tayari ulianza kuigombanisha Tanzania na nchi jirani ambao tayari maneno yalisambaa kuwa wapo tayari kutoa fedha ili uwekezaji huo ukafanyike katika nchi zao.
Ingawa Dk Bana hakuitaja nchi hiyo, lakini katika siku chache zilizopita, maneno kadhaa kupitia mitandao ya kijamii yalisambaa yakidai kuwa nchi ya Kenya ipo tayari kuhamishia uwekezaji huo kwao.
“Nampongeza sana rais wetu kwa kufanya jitihada za kusawazisha suala hili kwa kutoa fursa ya kuzungumza na Dangote, tunajua ana kazi nyingi lakini kwa kuwa ametambua umuhimu wa uwekezaji mkubwa uliofanywa na Dangote.”
Aliongeza kuwa kupitia mazungumzo na muafaka walioufikia utasaidia kupandisha thamani ya shilingi ambayo ilianza kuporomoka baada ya hali ya sintofahamu baina ya mwekezaji huyo na serikali.
Pia alisema kupitia mazungumzo hayo yaliyofanywa na rais inapaswa kuwa fundisho kwa wale wanaopenda kukwamisha maendeleo na kutaka kujinufaisha wao bila kuangalia athari ambayo taifa linapata na kufafanua kuwa, mazungumzo hayo yamemaliza upotoshaji wa wasiopenda maendeleo ya nchi.
“Haya ni maendeleo makubwa watanzania tusikubali kupotoshwa na wachache wasiopenda maendeleo hasa katika ushindani wa kibiashara kwani tukiendelea na upotoshaji huu tutakatisha tamaa wawekezaji wengine ambao wangependa kuwekeza jambo ambalo sio jema,” aliongeza Dk Bana.
Pia ametoa mwito kwa waandishi wa habari ambapo amewataka kufanya kazi zao kwa weledi na kuhakikisha kabla ya kutoa habari wafuatilie kwa kina ili kuepuka upotoshaji ambao unaweza kuleta athari kwa taifa.
“Tumeona habari ya Dangote imechochewa sana na waandishi wa habari ambao hawana weledi, niseme tu waandishi wanapaswa kuwa makini kwani kupitia kalamu zao wanaweza kuharibu,” alisema Dk Bana.
Mhadhiri mwingine wa Chuo Kikuu Ardhi ambaye hakuwa tayari kutaja jina gazetini, alisema vyombo vya habari vinapaswa kuweka uzalendo na weledi mbele katika kazi zao kwa kuwa ni watu muhimu kwa maendeleo ya taifa lolote.
"Inashangaza kuona baadhi ya vyombo vya habari vilikuwa vinashabikia nchi kupoteza mradi mkubwa kama ule, hawajui ni watoto wa kitanzania watakaokosa ajira, hili lisijitokeze tena, kuwe na uzalendo angalau kidogo kwa masuala kama haya," alisema mhadhiri huyo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Kigamboni, Dk Faustine Ndugulile amempongeza rais kwa jitihada zake na kutoa mwito kwa wanasiasa kuweka siasa pembeni hasa katika kuiletea nchi maendeleo ambayo yana manufaa kwa wananchi wake na taifa.
Alisema wapo watu waliotaka kujinufaisha na uwekezaji huo lakini hawakuangalia madhara yake endapo Dangote angeamua kusitisha uzalishaji kwani ungechangia kuleta hofu kwa wawekezaji wengine ambao wangetamani kuwekeza Tanzania.
“Siasa na uwekezaji ni mbalimbali ni vyema wanasiasa wakaweka vyama pembeni na kushiriki katika maendeleo ambayo rais wetu anapambana kila kukicha ili kuhakikisha Tanzania inafika katika uchumi wa viwanda,” alisema Dk Ndugulile.
Juzi Rais Magufuli alifanya mazungumzo na Dangote ambapo amemhakikishia mmiliki huyo wa kiwanda hicho kuwa serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri kwa wawekezaji na kumtaka mmiliki huyo kununua gesi moja kwa moja kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), badala ya kutumia watu wenye nia ya kutengeneza faida binafsi.
Magufuli alisema mradi huo uliingiliwa na wapiga 'dili' wakiwemo wanasiasa na kusema serikali haitaruhusu michezo hiyo na kwamba mianya yao imefungwa na wote waliohusika kutaka kuuvuruga, watashughulikiwa na serikali.
Dangote kwa upande wake alimhakikishia Rais Magufuli kuwa ataendelea kuwekeza katika ardhi ya Tanzania si tu kwa uwekezaji wa saruji lakini pia anafikiria kuwekeza pia katika sekta ya kilimo ili kushirikiana na Serikali kutokomeza tatizo la ajira.
Wadau Mtwara walonga Huko mkoani Mtwara, wafanyabiashara, wajasiriamali na wadau wa maendeleo wa mkoa humo wamesifu hatua iliyofikiwa na serikali na Dangote na kusema hatua hiyo imerejesha faraja kwao na matumaini mapya ya kuendeleza uchumi wa nchi.
Akiongea na gazeti hili, Mwenyekiti wa Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Kilimo (TCCIA) mkoani hapa, Saidi Swalla, alisema kuwa kusimama kwa kiwanda hicho kulizua hofu kwa uchumi wa mkoa na taifa kwa ujumla hivyo kuanza tena kwa uzalishaji kutaibua matumaini mapya kwao.
Alisema kutokana na kuwapo kwa mjadala uliokuwa ukiendelea katika vyombo vya habari ambao haukuwa na tija kwa uchumi wa mkoa na taifa kulileta hofu kwa wafanyabiashara ambao kwa kiasi kikubwa walishaanza kukitegemea kiwanda hicho katika kukuza uchumi wao.
“Ule mjadala haukuwa na tija kwa mkoa na taifa…lakini hatua hii ya serikali kukaa na mmiliki na kuja na suluhisho hakika kumerejesha matumaini mapya kwa wafanyabiashara na wadau wengine”, alisema Swalla.
Alibainisha kuwa tayari kuna wafanyabiashara ambao walishafungua maduka ya jumla na rejareja ya kuuza saruji ya kiwanda hicho katika maeneo mbalimbali mkoani hapa, lakini kusimama kwa uzalishaji kulisababisha maduka hayo yafungwe.
Mjasiriamali wa biashara ya chakula na vinywaji kwa ajili ya wafanyakazi wa kiwanda hicho kilichopo eneo la Hiyari, nje kidogo ya Manispaa ya Mtwara Mikindani, Anna Mkilanya, alisema kuwa alilazimika kufunga biashara yake kutokana na kukosa wateja baada ya kusimama kwa uzalishaji.
Alisema kuwa katika biashara yake anaajiri vijana na wasichana 12 lakini kutokana na kusimama kwa shughuli kiwandani hapo alilazimika kuwapunguza hadi kufikia wanne.
“Nilikuwa na vijana 12 hapa na biashara ilikuwa inachangamka vizuri lakini leo (jana) ndio kama unavyoona hapa. Hata hivyo tuliposikia Dangote kaleta malori zaidi ya 600 tumerudisha imani kuwa uzalishaji utaanza tena hivyo tunajipanga,” alisema mjasiriamali huyo aliyekutwa eneo la biashara yake na gazeti hili.
Mfanyabiashara wa vifaa vya ujenzi, Suleimani Khatani, alisema kuwa biashara ilikuwa ngumu kwa kuwa bei ya saruji ilipanda na wanunuzi waliokuwa wananunua kwa wingi kutoka huko vijijini walipotea.
Naye mjasiriamali na mwanachama wa umoja wa wafanyabiashara wanawake mkoani hapa, Virgilia Thomasi alisema kuwa serikali imefikia uamuzi mzuri na Dangote hasa katika kipindi hiki ambacho wakulima wameuza korosho kwa bei nzuri na kupata fedha za kutosha ili waweze kununua saruji kwa bei nzuri wajenge nyumba bora.
Alisema kabla ya kuanza kwa uzalishaji kiwanda cha Dangote bei ya saruji ilikuwa juu lakini kilipoanza bei ikashuka na kiliposimamisha uzalishaji bei ilirudi tena kuwa juu kama awali hivyo kufanya kasi ya ujenzi wa wa nyumba bora hasa vijijini kupungua lakini kwa muafaka huu wanamatumaini wataendelea na shughuli za ujenzi.
Malori mengine yaja Wakati wakazi wa mjini hapa juzi walishuhudia meli kubwa ikiwasili na kufunga gati katika Bandari ya Mtwara ikiwa na maroli 654 ambayo ni sehemu ya maroli 1,115 yanayoingizwa nchini na kampuni ya Dangote kwa ajili ya kusomba saruji na kusambaza nchi nzima, malori mengine 461 yanatarajiwa kuja siku chache zijazo.
Viongozi wa kiwanda hicho walisema kwa nyakati tofauti kuwa katika wiki mbili zijazo maroli mengine 461 yataingia ili kuwezesha usambazaji wa saruji hiyo kuwa rahisi zaidi kuliko ilivyokuwa hapo awali ambapo kampuni ilikuwa ikitumia maroli ya watu binafsi.
Ujio wa malori hayo umeibua upya matumaini ya wakazi wa Mtwara kuwa huenda katika kipindi cha hivi karibuni uzalishaji utaanza tena na hivyo bei ya saruji itashuka kutoka 16,500 ya sasa hadi ile iliyokuwa kabla ya kusimama kwa uzalishaji ambapo mfuko mmoja wa kilio 50 uliuzwa sh 11,000.
Wiki chache zilizopita kupitia mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari iliripotiwa kuwa kiwanda hicho cha Dangote kimesimamisha uzalishaji wa saruji kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo gharama za uendeshaji jambo lililofafanuliwa juzi katika kikoa cha Dangote na Rais Magufuli kuwa si kweli bali ni mbinu za wapiga dili kutaka kuharibu uwekezaji huo kwa maslahi binafsi.
Imeandikwa na Hassan Simba, Mtwara na Sophia Mwambe, Dar es Salaam.