Mtanzania mfanyabiashara maarufu na Rais wa Kampuni ya MeTL Group, Mohammed Dewji (MO) ,ameibuka mshindi wa tuzo ya Mtu aliyefanya vizuri katika Uongozi kwa Mwaka 2016 inayotolewa na Jarida la African Leadership.
Dewji ambaye ni miongoni mwa watu wakarimu Afrika aliibuka na ushindi huo kwa kupata kura asilimia 60.8 dhidi ya John Mahama,Rais mstaafu wa Ghana aliyepata kura 30.2 na kuwa mshindi wa pili.

Tuzo hiyo imeshindaniwa na watu zaidi ya 89,055 na kutazamwa na watu zaidi ya milioni 2.1 kwenye mtandao na nje ya mitandao kwenye Jukwaa la Jarida la African Magazine.
Kutangazwa kwa mshindi huyo kulitanguliwa na tathmini ya kura zilizopigwa na nyaraka zilizotumwa kupitia njia nyingine za mawasiliano na bodi na kamati ya uchaguzi wa mshindi wa tuzo hiyo iliypokuwa na wajumbe maalum kutoka wafanyabiashara wa Afrika, wanasiasa na viongozi wa kidiplomasia.
Dewji ameibuka mshindi katika kinyang’anyiro kikali kilichohusisha watu maarufa barani Afrika ikiwa ni pamoja na mwanzilishi wa kampuni ya ECONET Wireless,Mkenya,Chris Karubi,Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika,Akinwumi Adwesina,Naibu Rais, Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa na Waziri wa Mazingira wa Nigeria na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Aisha Mohammed.
Akizungumza katika hafla ya tuzo hiyo, Mchapishaji wa Jarida hilo, Dk. Ken Giami alisema ‘’Dewji anafaa zaidi kupata tuzo kwa sasa ili azishauri serikali juu ya masuala ya kutengeneza ajira katika bara la Afrika hususani kwa mafanikio aliyopata katika biashara na uongozi akiwa bado kijana.’’
Dewji atatunukiwa rasmi tuzo hiyo katika sherehe itakayofanyika Februari 24, mwaka huu katika Hoteli ya Southern Sun mjini Pretoria nchini Afrika Kusini.