MAHAKAMA ya Wilaya ya Maswa, Mkoa wa Simiyu imemhukumu Seleman Emanuel (21) mkazi wa Kijiji cha Sayusayu wilayani humo kwenda jela miaka 30 baada ya kupatikana na hatia ya kufanya mapenzi na mwanafunzi na kumsababishia ujauzito.

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo Fredirick Lukuna baada ya kuridhika na ushahidi uliotolewa mahakamani hapo na upande wa mashitaka bila kuacha shaka.
Akitoa hukumu hiyo, Hakimu huyo alisema kuwa anatoa adhabu hiyo ili liwe fundisho kwa watu wengine wenye nia mbaya ya kutaka kutenda kosa kama hilo katika jamii.
Awali ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka, Mkaguzi wa Polisi, Nassibu Swedy kuwa mshitakiwa alitenda kosa hilo mwezi Julai mwaka jana .
Mwendesha Mashitaka aliieleza Mahakama hiyo kuwa mshitakiwa alishirikiana kimwili na mwanafunzi huyo kike (jina linahifadhiwa) mwenye umri wa miaka 17 ambaye alikuwa Kidato cha Pili katika Shule ya Sekondari ya Isanga na kumsababishia ujauzito.