MAMA mzazi wa mtoto wa miezi minane na mganga wa kienyeji wanashikiliwa na Polisi kwa kuhusika na mauaji ya mtoto huyo aliyetambulika kwa jina la Rukia Joshua kwa lengo la kujipatia utajiri.
Imeelezwa kuwa mtoto huyo aliuawa kisha kutupwa katika tundu la choo cha Shule ya Msingi Chanela, katika kijiji cha Nassa, wilayani ya Busega, mkoani Simiyu.
Mama na mganga huyo wanashikiliwa katika kituo cha Polisi cha wilaya ya Busega kilichoko mjini Nyashimo.

Wakihojiwa na waandishi wa habari na wakazi wa kijiji hicho, mama huyo aliyetambulika kwa jina la Rusia Iluja alisema kuwa mganga wa jadi, Hewa Maduhu alimuua mtoto wake ili apate moja ya vichanganyio ambavyo vitatumika katika dawa mbalimbali ili vimpatie dawa ya utajiri.
Akisimulia zaidi Iluja aliwaambia waandishi wa habari kuwa, Maduhu aliingia ndani ya nyumba alipokuwa amelala saa 7 usiku, siku mbili kabla ya mwaka mpya na kumwingilia kimwili bila ridhaa yake huku akitishia kumuua kwa dawa alizonazo.
Wakati wa vitendo vyake hivyo vya kijahili, Iluja alisema Maduhu alimwambia ya kuwa mtoto wake ana mali kubwa katika mwili wake hivyo lazima amuue ili aweze kufanikiwa katika mambo yake.
Baada ya kusema na kumaliza ubazazi wake majira ya saa 9 usiku Maduhu alimchukua mtoto huyo na kwenda naye kwake huku akimwamuru asitoke nje na akitoka, atamfanyia kitu kibaya ambacho hajawahi kukifanya.
“Saa 10 alfajiri alikuja kuniambia eti Rukia amefariki na anaenda kumtupa na kunitaka nikae ndani tu atanikuta.
Alimchukua mke wake na kuelekea maeneo ya shule ya msingi Chanela huku nikiwafuata kwa nyuma bila ya wao kuniona mpaka walipomtumbukiza katika tundu la choo mtoto wangu,” alisema Iluja.
Alisema kuwa alikwenda katika kijiji cha Shigala ambacho anaishi mzazi mwenzake na kueleza mambo yote aliyofanyiwa na Maduhu na hivyo alimpeleka katika kituo cha Polisi Busega kutoa maelezo yake.
Katika mahojiano hayo, Maduhu alisema kuwa yeye kazi zake ni kuhakikisha anawasaidia wagonjwa ili wapone lakini anashangazwa na jambo hili la kuambiwa amemtupa mtoto chooni wakati mtoto huyo alipelekwa kwake kupata tiba.
“Ilikuwa ni kama siku 10 zilizopita nikiwa nyumbani kwangu nilipata wageni watatu ambao ni mama na watoto wawili huku mtoto mmoja ambaye ni Joshua mwenye umri wa miaka minne akiwa ni mgonjwa asiyejitambua nikaanza kumpatia dawa na kurejea katika hali yake huku mtoto mwingine (marehemu) naye akiwa anaumwa ila si sana,” alisema Maduhu.
Aliongeza kuwa alifanikiwa kurejesha hali za watoto hao na kuwa katika hali zao za kawaida za kila siku.
Aidha aliendelea kueleza kuwa siku moja baba wa mtoto alikwenda nyumbani kwake ili kulipa deni la tiba kwa mtoto wake lakini alipofika alidai kuwa kwa sasa hali yake si nzuri kipesa hivyo alimuomba ampe muda ili alipe deni hilo na alimkubalia kwa vile alikuwa anamfahamu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu, Onesmo Lyanga alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa uchunguzi unaendelea na utakapokamilika watuhumiwa wote watafikishwa mahakamani.