Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Mongella, akizungumza hii leo, kabla ya kukabidhi msaada wa vitanda 20, magodoro 20, vyandarua 20 pamoja na mashuka 100, uliotolewa na mbunge wa Viti Maalumu kupitia Chama cha Mapinduzi CCM mkoani Mwanza, Kemirembe Lwota.

Ameonya juu ya suala la uchafu kukithiri kwenye wodi za wagonjwa katika vituo vya kutolea huduma za afya ikiwemo hospitali ya rufaa ya Sekour Toure.


Mganga Mkuu mkoani Mwanza, Dkt.Leonard Subi, akizungumza kwenye utoaji wa msaada huo
Mbunge wa Viti Maalumu CCM mkoani Mwanza, Kemirembe Lwota, akizungumza wakati wa utoaji wa msaada huo
Mkuu wa Taasisi ya Mo Dewji, Barbara Gonzales, akizungumza wakati wa utoaji wa msaada huo
Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Mongella (kushoto), akimpongeza Mbunge wa Viti Maalumu CCM mkoani Mwanza, Kemirembe Lwota, baada ya kufanikisha upatikanaji wa msaada 

LakeFmHabari

Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Mongella, ameonya juu ya suala la uchafu kukithiri kwenye wodi za wagonjwa katika vituo vya kutolea huduma za afya ikiwemo hospitali ya rufaa ya Sekour Toure.

Mongella ametoa onyo hilo hii leo wakati akikabidhi msaada wa vitanda, magodoro, mashuka pamoja na vyandarua, uliotolewa na mbunge wa Viti maalumu kupitia Chama cha Mapinduzi CCM Mkoani Mwanza, Kemirembe Lwota.

Ameeleza kusikitishwa na hali ya uchafu katika wodi za wagonjwa hususani akina mama katika Vituo vya Afya, Zahanati pamoja na Hospitali huku akikuta mashuka mpya yamehifadhiwa stoo kwenye baadhi ya vituo hivyo.

“Na siyo hapa Sekour Toure tu, hata maeneo mengine, huwa nasikitika sana ninapokuta shuka chafu kitandani. Bahati mbaya nimewahi kwenda mahali nikakuta shuka mpya stoo, mimi nasema hizi shuka zitumike, zichakae, tutafute zingine”. Amesisitiza Mongella na kutaka suala la usafi kupewa kipaumbele zaidi.

Mganga Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Dkt.Leonard Subi, amesema huduma za afya zinaendelea kuboreshwa licha ya kuwepo uhitaji mkubwa wa vitendea kazi ambapo kwa siku yanahitajika mashuka manane kwa kila kitanda.

Mbunge wa Viti Maalumu CCM Mkoani Mwanza, Kemirembe Lwota, amewahimiza wadau wengine kujitokeza ili kusaidia kutatua kero za huduma za afya, huku akiishukuru taasisi ya Mo Dewji kwa kusaidia upatikanaji wa msaada huo ambao ni mashuka 100, vitanda 20, magodoro 20 pamoja na vyandarua 20 wenye thamani ya shilingi Milioni 25.

Mkuu wa Taasisi ya Mo Dewji, Barbara Gonzales, amesema taasisi hiyo imedhamiria kusaidia uboreshaji wa huduma mbalimbali katika nyanza za elimu, afya pamoja na maendeleo ya jamii ili kuboresha zaidi maisha ya wananchi.