TAASISI ya Tiba na Mifupa Muhimbili (MOI) imeishauri Serikali kuongeza uwezo katika hospitali zake za mkoa jijini Dar es Salaam, ama kujenga taasisi nyingine kama hiyo nne.
Hatua hiyo itapunguza msongamano wa majeruhi wa ajali wanaotibiwa hapo, ambao kwa siku ni wagonjwa 30.
Pia serikali imeshauriwa kuijengea taasisi hiyo utaalam wa kuelimisha wataalam zaidi katika kuhudumia majeruhi wa ubongo, uti wa mgongo, mishipa ya fahamu na viungo vikubwa kama nyonga na magoti.

Mkurugenzi wa Tiba wa MOI, Dk. Samuel Swai alitoa ushauri huo jana alipozungumza na Habari-Leo kuhusu wastani wa majeruhi wanaopokelewa kwa siku katika taasisi hiyo.
Dk Swai alisema kati ya wastani wa wagonjwa 30 wanaowapata kwa siku, 20 hadi 25 wanahitaji upasuaji.
Kati ya hao, walioumia vichwa ndani ya ubongo ni watano hadi 10, waliobaki wameumia sehemu mbalimbali za mwili ikiwemo mifupa mirefu, mikono, miguu, mifupa ya paja na nyonga.
Alisema walioumia migongo ni kati ya wawili hadi watatu, mmoja wao anaweza akawa amepoteza mawasiliano kwenye mikono na miguu au miguu peke yake.
“Kati ya majeruhi hao wa bodaboda ni 10 hadi 15, kati ya hao wameumia sana maeneo ya vichwa, migongo na miguu,” alisema Dk. Swai.
Akizungumzia watoto wanaofikishwa hapo, wengi wao wamevunjika viwiko, mguu wa paja au mikono.
“Sisi tunaamini wanaopata ajali ni wengi lakini wanaofikishwa hapa ni wale walioumia sana, wengine wanatibiwa huko huko kwenye hospitali za mkoa kama Hospitali teuli ya Tumbi, Mwananyamala na nyinginezo,” alisema.
Alisema hapo Moi wana meza mbili za upasuaji wa majeruhi kwa saa 24, lakini kuna siku wanapokea wagonjwa kati ya 60 hadi 100 kama kuna ajali ya basi.
“Kwa kuwa majeruhi wanakuwa wengi zaidi inatubidi wafunge meza za kawaida ziweze kuhudumia majeruhi” alisema.