Mwanamuziki mkongwe ambaye alipotea katika fani ya muziki kwa kipindi kirefu kutokana na matatizo ya dawa za kulevya, Rehema Chalamila “Ray C” ameibuka na kusema yupo fiti na ameachana na uteja.

Ray C ambaye amezungumza na ripota wa Globu ya Jamii katika studio za THT ambako yupo katika maandalizi ya kurekodi nyimbo ambazo zitamtambulisha upya katika ramani ya muziki wa bongo fleva.



“nakwambia niko fiti na tayari nimesharekodi nyimbo tano kwa mtayarishaji Johban John a nyingine nafanyia hapa THT kwa Imma the boy ambapo moja ya kazi yangu nimemshirikisha bushoke” amesema Ray C

Ray C amesema kuwa kwa sasa yeye ameamua kufanya muziki kama zamani na kamwe hawezi rudia kutumia dawa za kulevya kwani anajua zilivyomtesa kwa kipindi kirefu kiasi cha kushusha utu wake.
Amesema kuwa kwa sasa anachohitaji ni sapoti ya wadau wa muziki ambao wanaweza kumsaidia kuutoa muziki wake hapa ulipo na kuupeleka katika soko la kimataifa kwa kumsaidia kufanya video na mahitaji madogo madogo.

Ray C amewashukuru wadau mbalimbali ambao wamemsaidia mpaka kufikia hapo na kumtaja Ruge Mutahaba kuwa ni miongoni mwa watu waliopo katika mstari wa mbele kuakikisha yeye amekuwa sawa.