Mahakama mjini Nanjing, China, imewafunga jela wanaume wawili waliowatapeli wateja kupitia benki bandia, vyombo vya habari vya serikali vimeripoti.
Wanaume hao waliotambuliwa kwa majina Zeng na He, walipatikana na makosa ya kujipatia yuan 435m (£51m; $63m) kutoka kwa wateja 400.

Wamefungwa jela miaka tisa na miaka tisa unusu mtawalia.
Hukumu dhidi yao ilithibitishwa baada ya kesi dhidi yao kurudiwa, gazeti la People's Daily limeripoti.
Walianzisha chama cha ushirika ambacho afisi yake ndani zilifanana na za benki moja inayomilikiwa na serikali.
Walikuwa na madawati na makarani wenye sare zilizofanana na makarani rasmi wa benki ya serikali.
Hata stakabadhi za kuweka amana pesa kwenye benki zilikuwa sawa na za benki ya serikali.
Lakini ingawa taasisi hiyo ilikuwa na kibali cha kuhudumu kama chama cha ushirika, haikuwa na kibali cha kuhudumu kama benki.
Wahudumu waliwavutia wateja kwa kuwaahidi viwango vya juu vya riba kwa pesa walizoweka amana.
Shughuli haramu za taasisi hiyo ziligunduliwa mfanyabiashara aliyekuwa ameahidiwa riba ya juu alipodai riba aliyoahidiwa lakini akakosa kulipwa na akapiga ripoti kwa maafisa wa polisi mwaka 2014.
Ni baada ya hapo ambapo uchunguzi wa kina ulianzishwa.