Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Zelothe Steeven
MKUU wa Mkoa wa Rukwa, Zelothe Steven amemuagiza Kaimu Mganga Mkuu wa mkoa huo, Dk Emmanuel Mtika, ahakikishe mtoto Peter Kazumba (13) anayesumbuliwa na ugonjwa sugu wa ngozi, anapelekwa haraka katika Hospitali ya Mkoa wa Rukwa iliyopo Sumbawanga mjini kwa matibabu.

Mtoto Peter ambaye hasomi na hajawahi kuingia darasani anaishi na wazazi wake katika kitongoji cha Nkata kilichopo katika Kata ya Kate wilayani Nkasi, anasumbuliwa na ugonjwa sugu wa ngozi kwa zaidi ya miaka mitano bila kupona. Ugonjwa huo umemfanya aharibike na kutoa harufu kali, huku akiwa na jeraha kubwa la moto katika goti lake la mguu wa kushoto na anaonekana mzee kuliko umri wake.
Aidha, Zelothe aliwataka wakazi wa kitongoji hicho, kuacha kumnyanyapaa mtoto huyo pamoja na familia yake ya watu wote wanane, akiwemo baba na mama mzazi na watoto wengine watano akiwemo mtoto mwenye umri wa mwaka mmoja wameambukizwa ugonjwa huo. Zelothe alitoa maagizo hayo baada ya kufika katika kitongoji hicho na kujionea mwenyewe jinsi mtoto huyo anavyoteseka kwa kuugua ugonjwa huo, ambao madaktari wanadai hauambukizi.
Mkuu huyo wa Mkoa alilazimika leo kufunga safari hadi katika kitongoji cha Nkata, ikiwa ni siku moja baada ya gazeti hili kuripoti habari ya mtoto huyo na familia yake, ambayo imetengwa na wakazi wa kijiji hicho kwa hofu ya kuambukizwa.
Aliongozana na Kaimu Mganga Mkuu wa mkoa wa Rukwa, Mtika na Mratibu wa Ukoma na Kifua Kikuu mkoa wa Rukwa, Dk Dismas Buhiri. “Acheni kuinyanyapaa familia hii wala nisisikie wanaenda kutibiwa kwa mganga wa kienyeji, hivyo namuagiza Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa (Dk Mtika) aagize gari la wagonjwa lije kumchukua mtoto huyu haraka iwezekanavyo na kumpeleka kwa matibabu ya uhakika na uangalizi na uchunguzi wa kitabibu katika Hospitali ya Rukwa ya mkoa wa Rukwa iliyopo mjini Sumbawanga,” alisema.
Pia alimtaka Dk Mtika kuhakikisha anamtuma mtaalamu wa magonjwa ya ngozi kufika katika familia hiyo na kuwafanyia uchunguzi wa kitabibu, kubaini wanafamilia wengine wapatao saba kama wanaweza kutibiwa wakiwa nyumbani kwao; au kama watalazimika nao kutibiwa katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa. “Nataka maagizo yangu yatekelezwe haraka iwezekanavyo bila kuchelewa,“ alisema.
Alieleza kuwa anasikitika pia kusikia wazazi wa mtoto huyo, kuwa licha ya kumnyanyapaa, pia wanampiga mara kwa mara, hivyo kumwogopesha na kusababisha awe anatoroka nyumbani mara kwa mara na kushinda na kiu na njaa. “Inasikitisha sana kuwa licha ya mtoto huyu ambaye kweli ni mgonjwa sana na anateseka na ugonjwa, bado wazazi wanamnyanyapaa na kumpiga mara kwa mara, hii haikubaliki, lazima waache tabia hii ya kikatili mara moja,“ alieleza.
Aliwataka wakazi wa mkoa wa Rukwa, kuachana na tabia ya kuwaficha wagonjwa nyumbani kutokana na imani za kishirikina, bali wawahishe katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa matibabu. “Nawahimiza wakazi wa Kata ya Kate wajiunge na Mfuko wa Bima ya Afya ya Jamii (CHF) ili wasishindwe kutibiwa kwa kukosa fedha za matibabu, na nataka wakifika hospitali watibiwe haraka iwezekanavyo,“ alisisitiza.
Baba wa mtoto huyo, aitwae Martin Kazumba alimweleza Zelothe kuwa yeye ndiye alikuwa wa kwanza katika familia hiyo kuugua ugonjwa huo miaka saba iliyopita, kisha mke na watoto wote sita, walifuata kwa kuambukizwa ugonjwa huo. Kwa upande wake, mtoto Peter alikiri kuwa amekuwa akipigwa mara kwa mara na wazazi wake, hivyo analazimika kutoroka nyumbani hapo kwa kuogopa vichapo.
Kwa upande wake, Dk Mtika alieleza kuwa baada ya kumwona mtoto Peter, upo uwezekano mkubwa kwamba ugonjwa alionao ni wa ngozi au upo uwezekano kuwa familia hiyo imekula chakula, ambacho kimewasababishia mzio (allergy) na siyo ugonjwa ambao unaweza kuambukiza. Akifafanua, alieleza kuwa huo sio ugonjwa wa kuambukiza kwa sababu hakuna watu wanaoishi karibu na familia hiyo, wameambukizwa ugonjwa huo.
“Mtoto Peter anaumwa, hali yake sio nzuri, kwanza amedhoofika kwa njaa na kiu, mbaya zaidi anajikuna sana mwili mzima, hii inaonesha kuwa hapati usingizi wa kutosha, amechanganyikiwa, isitoshe ugonjwa huo umeharibu vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake. Pia hatembei vizuri, anatembea kwa kuchechemea, jambo ambalo sio zuri, wataalamu wa ngozi wapo, vifaa na dawa vipo, tutampeleka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wetu ambapo atakuwa chini ya uangalizi wa wataalamu hao isitoshe atafanyiwa uchunguzi wa kitabibu,“ alisisitiza.
Mratibu wa Ukoma na Kifua Kikuu wa Mkoa wa Rukwa, Dk Buhili aliwatoa hofu wakazi wa kitongoji hicho kuwa ugonjwa ulioikumba familia hiyo, sio ugonjwa wa ukoma. Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nkata, Wilbroad Feruzi alisema anawashukuru viongozi wa mkoa huo kwa kufika katika eneo hilo na kushuhudia wenyewe jinsi mtoto Peter anavyoishi na kutoa msaada wa kumsafirisha hadi mjini Sumbawanga kwa matibabu na uchunguzi wa kitabibu.
Mtoto Peter aliokotwa na Paroko wa Kanisa Katoliki lililopo katika Kata ya Kate, Padre Jofrey Kitaya, asubuhi ya Jumatatu ya Pasaka akiwa amelala usiku kucha pembezoni mwa zahanati ya Mtakatifu Anna, inayomilikiwa na watawa wa Kanisa Katoliki iliyopo katika kijiji cha Kate.
Padre Kitaya alidai kuwa alipomhoji mtoto huyo, alimweleza kuwa amelazimika kutoroka nyumbani kwao na kutembea kwa miguu umbali wa kilomita nne baada ya kupigwa na wazazi wake na pia alidai kuwa anawahofia wazazi wake hao. Kitongoji cha Nkata kipo umbali wa kilomita 64 kutoka mjini Sumbawanga.