Takriban watoto 20 wamefariki katika ajali ya barabarani katika mkoa wa Mpumulunga nchini Afrika Kusini kaskazini mwa mji mkuu wa Pretoria.
Kulingana na chombo cha habari cha Reuters, basi dogo walilokuwa wakisafiria liligonga lori na kulipuka.

Russel Meiring ,ambaye ni msemaji wa shirika la matibabu ya dharura ER24 ameambia Reuters kwamba watoto 20 walikuwa ndani ya basi hilo wakati lilipogongana na lori hilo la kubeba mizigo.
''Idadi hiyo sasa inadaiwa kufika 20'', alisema.
Chapisho la awali ambalo lilithibitisha watoto 13 kufariki ilionyesha eneo la ajli hilo.
Panyaza Lesufi, afisa anayehusika na elimu katika mkoa wa Gauteng amesema kuwa ni 'siku nyeusi'.
Wamedaiwa kuwa wanafunzi wa shule ya msingi na ile ya upili.
Haijajulikani ni nini haswa kiini cha ajali hiyo, lakini picha zinaonyesha basi hilo lilichomeka kabisa.
Baada ya moto kuzimwa, maafisa wa matibabu walipata watoto 13 wakiwa wamekwama ndani ya gari hilo.
''Hawakuweza kunusurika na wakatajwa kuwa walifariki papo hapo'', taarifa hiyo ilisema.
ER24 na idara ya elimu katika mkoa wa Gauteng zimethibitisha kwamba watu 20 walifariki.