Sekta ya utalii nchini Kenya imepigwa jeki baada ya rais Uhuru Kenyatta kufungua hoteli mbili mbali na kuzindua ujenzi wa jumba refu barani Afrika.
Hoteli hizo mbili zitakazojulikana kwa jina Nairobi Hotels, ni hoteli ya Park Inn iliopo eneo la Westlands iliyo na vitanda 140 na kusimamiwa na Radisson Hotel na Lazizi Premier ilio na vitanda 144 na itakuwa hoteli ya kwanza ya kifahari itakayokuwa karibu na uwanja wa ndege.

Rais pia aliweka jiwe la msingi la Jumba la Pinnacle Tower ambalo litakuwa refu zaidi barani Afrika.
Jengo hilo litakalojengwa katika eneo la Upper Hill jijini nairobi, litakuwa na ghorofa 70 na urefu wa futi 900 hivyobasi kulifanya kuwa refu zaidi barani.
Jumba hilo litakuwa na ofisi za kibiashara nyumba za kukodisha na Hoteli ya Hilton Hotel mbali na kuwa na duka la jumla na kituo cha burudani.
Kwa sasa jumbe refu zaidi barani Afrika ni lile la Carlton Center lililopo mjini Johannesburg nchini Afrika Kusini.
Limekuwa jumba refu zaidi kwa kipindi cha miaka 39 hadi kufikia sasa.
Jumba la Pinnacle Towers litakuwa miongoni mwa majumba marefu duniani.
Jumba la Dubai Burj Khalifa ndio refu zaidi duniani likiwa na urefu wa mita 800.
Rais Uhuru kenyatta akionyeshwa picha za jumbe hilo refuHaki miliki ya pichaIKULU YA RAIS NAIROBI
Image captionRais Uhuru kenyatta akionyeshwa picha za jumbe hilo refu
Majumba mengine marefu duniani ni Eiffel Tower lililopo mjini Paris ambalo halijafikia urefu wa mita 300, Jumba la Time Warner lililopo mjini New York na lenye urefu wa mita 200 na lile la Gherkin mjini London lenye urefu wa mita 180.
Kwa sasa Jumba la UAP Old Mutual jijini Nairobi ndio jumba refu zaidi katika eneo la Afrika ya mashariki likiwa na ghorofa 33 na urefu wa mita 163.
Linafuatiwa na Jumba la Twin Tower mjini Dar es salaam lenye ghrofa 35 na urefu wa mita 153.
Jumba hilo la Kenya linatarajiwa kukamilika mnamo mwezi Disemba mwaka 2019, ijapokuwa hoteli yenye vyumba 255 itakamilishwa mapema.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Rais Uhuru Kenyatta alipongeza uwekezaji huo akisema kuwa hautabuni ajira pekee kwa Wakenya bali pia utabadilisha anga ya mji mkuu wa Nairobi.
Aliwahakikishia wawekezaji kuhusu azma yake ya kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji nchini humo.
''Tutashirikiana na sekta ya kibinafsi kubuni ajira.Kile tunachotaka ni kazi kwa watu wetu'', alisema Kenyatta wakati alkipofungua hoteli ya partk Inn iliopo eneo la Westlands.
Akiweka jiwe la msingi la jumba hilo refu, rais Kenyatta amesisitiza kuwa uwekezaji mkubwa unaoendelea unaonyesha wazi kwamba utalii wa Kenya unaendelea kuimarika baada ya kudorora kwa kipindi kirefu.