Jeshi la Polisi Zanzibar limesema kuwa limekamilisha kumhoji msichana aliyejitosa bahari ya hindi eneo la Chumbe alipokuwa akisafiri na boti ya Azam Kilimanjaro V kutoka Dar es Salaam kwenda Zanzibar.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Hassan Nasir Ali alisema msichana huyo anayesoma kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari Glorious pamoja na watu wengine, tayari wameshahojiwa kutokana na tukio hilo lililotokea Aprili 3 mwaka huu.
Baada ya upelelezi kukamilika, muda wowote jalada hilo litafikishwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) ili hatua zaidi za kisheria ziweze kuchukuliwa.
Wakati Polisi wakikamilisha upelelezi, Mratibu wa Huduma za Afya Mjini Unguja, Suleiman Abdi Ali alisema msichana huyo aliathirika kisaikolojia hivyo isingekuwa vizuri kwa yeye kuhojiwa wakati huu.