Rais wa Zimbabwe Robert Mugabe amesafiri kwenda Singapore kufanyiwa uchunguzi wa kimatibabu, gazeti la serikali la Herald limeripoti.
Kiongozi huyo wa umri wa juu zaidi duniani, ambaye amekuwa akionekana dhaifu hadharani siku za karibuni, alihutubia wajumbe katika mkutano mkuu wa Baraza la uchumi Duniani Afrika Kusini wiki iliyopita.

Shirika la habari la AFP linasema alihutubia "kwa sauti hafifu huku akiwa amejibwaga kwenye kiti".
Gazeti la Herald linasema amekwenda Singapore kwa "uchunguzi wake wa kawaida wa kimatibabu".
Bw Mugabe anatarajiwa kurejea nyumbani kwa wakati kuweza kuhudhuria mazishi ya jaji mkuu wa zamani Godfrey Chidyausiku.
Makamu wa Rais Emmerson Mnangagwa atatekeleza majukumu ya rais Bw Mugabe atakapokuwa nje ya nchi hiyo.
Licha ya umri wake, chama tawala cha Zanu-PF kilimuidhinisha Bw Mugabe kuwa mgombea urais wa chama hicho katika uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.
Katika mkutano Februari, mkewe, Grace Mugabe, alisema: "Siku moja Mungu atakapoamua kwamba Mugabe afe, basi tutakuwa na maiti yake kama mgombea kwenye karatasi ya kura."
Bw Mugabe ameongoza taifa hilo tangu uhuru mwaka 1980.