Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya maombi ya shukrani kitaifa na kuiombea nchi na Rais Dk. John Magufuli , Askofu Mkuu wa Naoith Pentekoste Church, Dk.David Mwasota (katikati), akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, kuhusu maombi hayo yatakayofanyika Julai 15 mwaka huu Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam. Kulia  ni Askofu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God Jimbo la Dar es Salaam, Lawrence Kameta   na kushoto ni Mratibu wa mkutano huo ambaye ni Askofu Mkuu wa Kanisa la Abudant Blessing Center (ABC), Askofu Flaston Ndabila. 


 Mratibu wa mkutano huo ambaye ni Askofu Mkuu wa Kanisa la Abudant Blessing Center (ABC), Askofu Flaston Ndabila (kushoto), akizungumza kwenye mkutano huo. 
Askofu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God Jimbo la Dar es Salaam, Lawrence Kameta, akisisitiza jambo kwenye mkutano huo.


Mjumbe wa kamati ya maandalizi ya mkutano huo, Jane Magigita, akizungumza kwenye mkutano huo. 

Wanahabari wakichukua taarifa hiyo.


Na Dotto Mwaibale

WAZIRI wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba anatarajiwa kuongoza viongozi wa Serikali, kidini na wananchi katika maombi maalum ya shukrani ya kuiombea nchi pamoja na Rais Dk. John Magufuli ili aweze kuendelea kufanyakazi zake.

Akizungumza na Waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya maombi hayo, Askofu Mkuu wa Naoith Pentekoste Church, Dk.David Mwasota amesema, maombi hayo yatafanyika Julai 15, mwaka huu katika Uwanja wa Uhuru.

Alisema katika maombi hayo yaliyoandaliwa na viongozi wa dini kutoka madhehebu mbalimbali, I Go Africa For Jesus na wananchi yatatoa fursa ya kuiombea amani nchi.

"Hadi sasa kuna wenzetu kutoka nje ya nchi Marekani wameomba.kushiriki nasi na tutakuwa pamoja nao wametaka waje wengi lakini imebidi tuweke ukomo,"alisema Mwasota.

Alisema lengo kuu la maombi hayo pia ni kumuunga mkono Rais Dk.Magufuli ambaye amekuwa akiomba watanzania wamuombee mara kwa mara.

Mwasota alisema kabda ya maombi hayo kutakuwa na semina kwa ajili ya siku mbili ya viongozi hao kama maandalizi ya siku hiyo maalum ya maombi.

Mratibu wa mkutano huo ambaye ni Askofu Mkuu wa Kanisa la Abudant Blessing Center (ABC), Askofu Flaston Ndabila  alisema, pia kila mkoa utawakilishwa na mjumbe mmoja katika maombi hayo.

Alisema baada ya maombi hayo kila mkoa utaendelea na maombi yake kulingana na ratiba zao ambapo aliwataja baadhi ya maaskofu watakaohudhuria maombi hayo kuwa ni  ni Dk. Philemon Tibananason, Dk.Bernard Mwaka, Sylvester Gamanywa, Lawrence Kameta, Dk.Barnabas Mtokambali na wengine kutoka nje ya nchi.

Alisema waandaaji wa maombi hayo ni Nyumba ya Maombi Tanzania Igo Africa For Jesus na viongozi wa makanisa wa huduma za kikristo Tanzania.

Askofu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God Jimbo la Dar es Salaam, Lawrence Kameta ambaye anatoka kanisa la  Tabata, alisema shughuli zote za maombi hayo zimepata baraka kutoka uongozi wa juu wa umoja wa  makanisa yaliyoungana kufanya maombi hayo ya kihistoria hapa nchini.


(Imeandaliwa na mtandao wa www.habari za jamii.com-simu namba 0712727062)