Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angela Kairuki
SERIKALI imetangaza neema kwa halmashauri zote nchini ikisisitiza kuwa watumishi watapandishwa vyeo na ajira mpya zitatolewa kujaza nafasi za wote waliogundulika kuwa na vyeti feki.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angela Kairuki alisema hayo jana jijini Dar es Salaam alipokutana na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke kusikiliza changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi.

Alisema sasa serikali imepanga kutoa ajira maalumu kwa kila halmashauri ili kujaza nafasi za watumishi walioondolewa kazini baada ya kubainika kugushi vyeti pamoja na wengine waliokuwa na vyeti feki.
“Nikianzia na Halmashauri ya Temeke, niwahakikishie kuwa tatizo la watumishi litapungua na pia kwenye kila manispaa iliyoondokewa na wafanyakazi kwa sababu ya vyeti feki, watapewa idadi ileile ya watu ili waweze kujaza nafasi zao na hivyo, kuziba mapungufu waliyoyaacha,” alisema Waziri Kairuki. Alisema zaidi ya watumishi 133,000 wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke watapandishwa vyeo katika kipindi cha Mwaka wa Fedha wa 2017/18.