Vijana 6 wa Burundi watoweka katika mashindano Marekani

Vijana sita wa Burundi waliokuwa wakishiriki katika mashindano ya roboti nchini Marekani wameripotiwa kutoweka, polisi wanasema.
Wavulana wanne na wasichana 2 walio kati ya umri wa miaka 16 na 18 walipotea wakati wa mashindano hayo ya kwanza duniani yaliofanyika Washington DC.

Idara ya polisi mjini humo imesema kuwa mara ya mwisho vijana hao kuonekana ilikuwa siku ya Jumanne wakati wa makamilisho ya michezo hiyo.
Ripoti zinasema kuwa vijana wawili kati yao tayari wamevuka mpaka na kuingia Canada lakini ripoti hiyo haijathibitishwa na polisi.
Siku ya Alhamisi, idara ya polisi mjini humo ilibandika picha za sura za vijana hao sita waliopotea katika mtandao wao wa Twitter, wakiwataka raia kuwasiliana nao iwapo watakuwa na habari yoyote kuwahusu.
Vijana hao wanatambulika kuwa Don Ingabire, Kevin Sambukiza, Nice Munezero, Audry Mwamikazi, Richard Irakoze na Aristide Irambona.
Waandalizi wa mashindano hayo wanasema kuwa waliwaeleza polisi baada ya msimamizi wa timu hiyo ya Burundi kushindwa kuwapata vijana hao.
Katika taarifa , msemaji wa mashindano hayo Jose Escotto alisema, ripoti kamili imewasilishwa kwa polisi ambao wanachunguza kisa hicho, kulingana na gazeti la The Washington Post.
Mashindano hayo ya siku 3 yalihudhuriwa na timu 150 zilizokuwa zikishindana.
Mashindano hayo yanalenga kuwashawishi vijana kukuza vipaji vyao katika masomo ya sayansi, technolojia, uhandisi na hesabu.