Wanachama wa Shirika la Africa Diaspora Forum wamefanya mandamano nchini Afrika Kusini kushinikiza serikali ya nchi hiyo na serikali ya Tanzania kubaini ukweli kuhusu kuuawa kwa mwanafunzi raia wa Tanzania mwezi jana.
Bw Baraka Leonard Naferi, mwanafunzi wa shahada ya uzamifu, alifariki baada ya kugongwa na gari la teksi nje ya bweni la chuo kikuu.
Maafisa wa shirika hilo wameandamana kwa pamoja nabaadhi ya wanafunzi na wafanyakazi wa Chuo Kikuu cha Johannesburg nje ya bweni kwa jina Sophiatown ambapo mwanafunzi huyo aligongwa na kuuawa.
Yalikua maandamano salama na watu walikusanyika kwenye uzio wa seng'enge pahala gari lilipo mgonga marhem Baraka Naferi wakiwa wamebeba mabango yanayosema tunataka haki kwa Baraka, haki itendeke kwa Baraka.
Maua kwenye uzio
Mshukiwa alikamatwa na polisi wa Afrika Kusini lakini baadaye akaachiliwa huru kwa dhamana.
Polisi walisema hakukuwa na ushahidi wa kutosha wa kumfungulia mashtaka ya mauaji.

Badala yake, Mwandishi wetu Omar Mutasa aliyeko Johannesburg anasema polisi walimfungulia mashtaka ya kuendesha gari bila leseni.
Waandamanaji walitoa wito kwa polisi mtuhumiwa arejeshwe korokoroni.
Waliweka shada la maua kwenye uzio wa bweni la Sophiatown alipouawa Bw Baraka.
Mkuu wa Africa Diaspora Forum Marc Bafou ameitaka serikali ya Afrika Kusini na serikali ya TZ pamoja na wakuu wa chuo kikuu cha Johannesburg mauaji haya wayape kipao mbele maana yatazidi kukiaibisha chuo kikuu cha Johannesburg na taifa la Afrika Kusini, mauaji yalioonekana kama chuki dhidi ya raia wa kigeni.
Africa Diaspora Forum imesema Tanzania inafahamu fika gharama ya kumpata mwanafunzi mmoja aliyehitimu shahada ya udaktari kwa hivo serikali ya Tanzania isiliachie suala hili kwa wepesi.
Mwandishi wetu anasema marafiki zake Bw Baraka waliosoma naye na pia kufanya kazi naye wamesema alikuwa mtu mzuri sana na hata mwanamke mmoja mweupe alizungumza kwa Kiswahili na kusema watu waliomuua Baraka Naferi hawana utu hata kidogo.
Wengine kutoka DRC walisema mauaji haya ya Baraka sio tatizo la Afrika Kusini na Tanzania pekee yake lakini ni tatizo la Jumuia ya SADC kulitatua kwa raia wanaotoka mataifa mengine ya SADC wanaosoma katika vyuo vikuu vya Afrika Kusini .
Bw Baraka aliuawa mnamo 23 Februari.
Baadhi ya wanafunzi wanasema kuna kanda ya video za usalama ambayo inamuonesha mwanafunzi huyo akikimbia na mwanafunzi mwingine, nyuma wakiandamwa na watu wawili waliokuwa ndani ya gari la teksi.
Gari hilo linaonekana kuwakimbiza na hatimaye Baraka anagongwa mara kadha akiwa kwenye uzio wa bweni.