Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Kinywa, Mataya na Uso wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dkt. Doraha Kiwale (kulia), Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Kinywa, Mataya na Uso, Dkt. Daud Shaban wa Muhimbili (katikati) na Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Kinywa, Mataya na Uso, Dkt. Baraka Kileo wa Muhimbili wakifanya upasuaji wa kuondoa uvimbe chini ya shingo ya mgonjwa ambao umeziba mshipa mkubwa wa kupeleka damu kwenye ubongo. Wa pili kutoka kulia ni Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Kinywa, mataya, na Uso, Prof. Thaer Raifallah kutoka Hospitali ya Kansas City na Chuo Kikuu cha Missouri huko Marekani akishiriki kwenye upasuaji huo. 
Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Kinywa, Mataya na Uso wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dkt. Daud Shaban akizungumza na mwandishi wa habari kuhusu upasuaji wa kinywa, mataya na uso ambao unafanywa na wataalam wa Muhimbili kwa kushirikiana na wataalam kutoka Hospitali ya Kansas City na Chuo Kikuu cha Missouri nchini Marekani. 
Wataalam wa wakiendelea na upasuaji katika hospitali hiyo.

Wataalam wabobezi wa upasuaji wa kinywa mataya na uso (Oral & maxillofacial surgeons) wa Hospitali ya Taifa 


Muhimbili (MNH) kwa kushirikiana na wenzao wa Marekani kwa mara ya kwanza kupitia Hospitali ya umma nchini, wamefanya upasuaji wa ubingwa wa kuunganisha mifupa ya fuvu kwa mgonjwa aliyepata ajali na sura yake kuharibika.

Upasuaji huo ambao ulifanywa na wataalam wa Muhimbili kwa kushirikiana na wenzao kutoka Hospitali ya Kansas City na Chuo Kikuu cha Missouri nchini Marekani, ulifanikiwa kurejesha sura ya mgonjwa huyo katika hali yake ya kawaida.

Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Kinywa, Mataya na Uso, Dkt. Daud Shaban amesema upasuaji mwingine uliofanyika unahusisha wagonjwa waliokuwa na uvimbe mkubwa sehemu ya taya na uso. Amesema pia wataalam wenzake walifanya upasuaji wa kutengeneza taya jipya kwa mgonjwa aliyepata ajali na taya lake kuharibika ambapo wamechukua kipande cha mfupa kutoka kwenye sehemu ya kiuno chake na kukiunganisha na taya ili kulikamilisha upasuaji huo.

Katika hatua nyingine, watalaam hao wamefanikiwa kuondoa uvimbe chini ya shingo ambao ulikuwa umeziba mshipa mkubwa wa damu wa kupeleka damu kwenye ubongo. “Uvimbe huo ulisababisha mgonjwa kuumwa kichwa kwa muda mrefu na kumsababishia dalili za kiharusi, kuzimia mara kwa mara na kupoteza kumbukumbu. Hakuna shaka kwani baada ya uvimbe kuondolewa, sasa mgonjwa ataendelea na maisha yake ya kawaida vizuri,” amesema Dkt Shaban.

Amesema ujio wa watalaam hao umeowaongezea ujuzi wa kuendelea kufanya upasuaji mkubwa kwa wagonjwa wenye matatizo mbalimbali kutoka kila pembe ya Tanzania. “Pia, wameleta msaada wa vifaa tiba vyenye thamani ya Tshs. 250 milioni ambavyo vitaendelea kutumiwa na watalaam wa MNH kutoa huduma kwa wagonjwa wenye matatizo hayo,” amesema daktari huyo.

Vifaa hivyo ni pamoja na mashine za kuchimbia mifupa kwenye mashimo ya taya na vyuma vya kufungia taya na mifupa iliyovunjika, nyuzi za kushonea wagonjwa baada ya upasuaji pamoja na dawa mbalimbali. Upasuaji wa wagonjwa hawa ungegharimu kiasi cha Tshs. 420 milioni kama wangeenda kutibiwa nje ya nchi.