KLABU ya Real Madrid imemtangaza Zinedine Zidane kuwa Kocha Mkuu wa Klabu hiyo ikiwa ni miezi 10 tu tangu Mfaransa huyo alipobwaga manyanga kuitumikia miamba hiyo ya Santiago Bernabeu.

Zidane mwenye umri wa miaka 46 ambaye ameiongoza Madrid kuchukua ubingwa wa UEFA mara tatu mfululizo, amechukua mikoba ya Santiago Solari aliyeifundisha timu hiyo kwa kipindi kisichozidi miezi mitano na sasa amesaini mkataba utakaomuweka klabuni hapo hadi mwaka 2022.


Solari alitimuliwa kazi hapo jana baada ya ushindi wa ugenini wa mabao 4-1 dhidi ya Real Valladolid kufuatia kipigo cha kushtukiza kutoka kwa Ajax kwenye michuano ya UEFA ambacho kiliwasukuma nje mabingwa hao watetezi.
Zidane alibwaga manyanga baada ya mechi ya fainali ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya Liverpool ambapo waliibuka mabingwa kwa ushindi wa mabao 3-1 huku Julen Lopetegui akiajiriwa kuchukua mikoba yake kabla ya Kombe la Dunia na kisha kutimuliwa miezi minne baadae ambapo Santiago Solari alichukua mikoba yake kama kocha wa muda kabla ya kupewa mkataba hadi mwaka 2021.

Zidane ataanza kibarua chake kipya siku ya Jumamosi ambapo kikosi cha Real Madrid kitashuka dimbani Santiago Bernabeu kuwavaa Celta Vigo kwenye LaLiga akiwa na kazi ya ziada kuwafukuzia Barcelona waliopo kileleni kwa tofauti ya alama 12 dhidi ya kikosi cha Los Blancos waliopo katika nafasi ya tatu.