KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John  Mnyika, “ameutema rasmi” ubunge wake, katika jimbo la Kibamba jijini Dar es Salaam.

Mnyika ambaye amekuwa mbunge wa Kibamba ambayo ilikuwa sehemu ya jimbo la Ubungo, kwa miaka kumi mfululizo, hayumo katika orodha ya wanachama wa Chadema waliopigiwa kura za maoni, kutaka kuteuliwa kugombea nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020.


Hakuna taarifa zozote zinazoeleza sababu za mwanasiasa huyo, kutogombea tena nafasi yake hiyo.
Hata hivyo, baadhi ya washindani wake ndani ya Chadema wanasema, mbunge huyo ameamua kutogombea nafasi yake hiyo, kwa kuhofia kushindwa katika uchaguzi mkuu.

Wakati baadhi wakidai hivyo, taarifa zinasema, hatua ya Mnyika kujiweka kando katika kinyang’anyiro hicho, imetokana na kubanwa na majukumu ya nafasi yake ya ukatibu mkuu.

Mnyika alichaguliwa kuwa katibu mkuu wa chama hicho Desemba mwaka 2019 akichukua nafasi ya Dk. Vincent Mashinji ambaye jina lake halikupendekezwa na Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa chama hicho, ili kuidhinishwa na wajumbe wa Baraza Kuu la chama hicho.