BAADA ya kupoteza kwa bao 3-2 katika mchezo uliopita dhidi ya Mbao FC, Mabingwa wa Ligi Kuu Soka Tanzania Bara, Simba Sports Club leo imerejesha Kikosi chake chote na kuilaza Alliance FC bao 5-1 katika dimba la Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Simba SC kama kawaida yao walianza mchezo huo kwa kasi zaidi wakiwa na Nyota wao machachari, Cloutous Chama, Meddie Kagere , Luis Miquissone, Gerson Fraga Vieira na wengine wengi ilitandaza kabumbu safi na kupata mabao hayo katika mchezo huo wa mwisho kwa Klabu hiyo kucheza Dar es Salaam.


Mabao ya Simba katika mchezo huo yalifungwa na Mshambuliaji, Meddie Kagere dakika ya 23 kwa mkwaju wa Penalti na bao la pili dakika ya 44, bao la tatu lilifungwa na Luis Jose Miquissone dakika ya 64 kwa 'chopping' safi nje kidogo ya 18 za lango la Alliance FC, bao la nne lilifungwa na Winga Deo Kanda dakika ya 75 baada ya krosi safi kutoka kwa Shomari Kapombe wakati bao la tano likiwekwa kambani na Kiungo Saidi Hamis Ndemla dakika ya 86. Alliance walipata bao lao kupitia kwa Martin Kigi dakika ya 39.

Mchezo huo ni mchezo wa mwisho kwa Simba SC kucheza hapa jijini Dar es Salaam ikiwa ni ishara ya kuwaaga Mashabiki wake katika jiji hilo msimu huu wa 2019-2020. Baada ya hapo Simba itasafiri hadi mkoani Tanga kwa ajili ya mchezo wake dhidi ya Coastal Union na Moshi kwa mchezo dhidi ya Polisi Tanzania.

Hitimisho la michezo hiyo ya Ligi Kuu msimu huu na kuipa Simba SC Ubingwa wa Ligi hiyo, August 2, mwaka huu watakuwa na kibarua kizito dhidi ya Namungo FC katika mchezo wa Fainali ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup) msimu wa 2019-2020, mchezo utaopigwa kwenye dimba la Nelson Mandela, mkoani Rukwa.