Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta(Kushoto) alifanya ziara binafsi ya siku mbili nchini Tanzania mwaka 2019

Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta amemtumia salamu za heri kwa rais mwenzake wa Tanzania John Pombe Magufuli kwa kushinda uchaguzi uliomalizika hivi punde.

Rais Kenyatta amesema kuchaguliwa tena kwa Magufuli ni ishara ya upendo na imani waliyo nayo Watanzania kwa uongozi wake.

"Kwa niaba ya Watu, Serikali ya Kenya na Mimi mwenyewe nampongeza ndugu yangu, Dkt John Pombe Magufuli kwa ushindi wako na wa Chama Cha Mapinduzi, katika uchaguzi uliomalizika", alisema rais Kenyatta.

Aliongeza kuandika: ''Nchi ya Kenya inatarajia kuendelea kufanya kazi na Utawala wako kwa faida ya watu wa mataifa yetu mawili, kwa ustawi wa Afrika Mashariki na kwa amani, utulivu na ukuaji wa bara la Afrika.

Rais Kenyatta pia amemtakia rais mwenzake wa Tanzania afya njema na ufanisi anapojiandaa kuhudumu kwa muhula wa pili madarakani na kumhakikishia ushirikiano wa Kenya na kwa utawala wake .

k

Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli ametetea nafasi yake baada ya kushinda kwa kishindo Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumatano wiki hii.

Magufuli ameshinda kwa kupata kura 12,516,252 ambayo ni asilimia 84 ya kura zote zilizopigwa.

Tundu Lissu kutoka chama cha upinzani cha Chadema ameshika nafasi ya pili kwa kupata kura 1,933,271 ya kura zote ziizopigwa.

Jumla ya watu 15,91950 walipiga kura hizo wakati waliojiandikisha kupiga kura walikuwa 29,754,699 kwa mujibu wa Tume ya taifa ya Uchaguzi (NEC).

Hata hivyo vyama vikuu vya upinzani wamekataa matokeo ya uchaguzi huo wakidai uligubikwa na udanganyifu.

Uchaguzi huu ambao Magufuli alikuwa akiwania nafasi hiyo ya juu alikuwa na washindani wengine 14.