Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimemtaka Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson kuwaondoa bungeni wabunge 19 wa viti maalum kikidai ni  'haramu' na kwamba uamuzi huo ndio takwa la kikatiba.


Kauli hiyo imetolewa  leo Jumapili Juni 26, 2022 na Spika wa Bunge la wananchi la chama hicho, Celestine Simba alipozungumza na vyombo vya habari.

Amesema Chadema haijapokea wito wala taarifa yoyote kutoka mahakamani kuhusu kufunguliwa kwa zuio au kesi mpya inayowapa haki wanachama hao kubaki bungeni.

"Kuhusu uamuzi wa mahakama wa Juni 22, 2022 tayari tumeshapokea nakala ya hukumu na tumeiwasikisha Tume ya Taifa ta Uchaguzi (NEC) na Bungeni kusisitiza kuondolewa kwa wabunge hao haramu," amesema Celestine.

Pia, kimeishauri  CCM kukaa mezani na Spika Dk Tulia kwa kile walichodai 'kumpa somo' kiongozi huyo wa Bunge namna ya kukiongoza chombo hicho.

Juni 22, 2022 Mahakama Kuu ilitupilia mbali zuio la wabunge hao baada ya hoja mbili kati ya sita za pingamizi zilizowasilishwa na Chadema kubaini dosari za kisheria katika zuio hilo.