Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mh Paul Christian Makonda amefanya ziara ya kutembelea maeneo yaliyopata athari ya mvua kubwa huku akiwataka wananchi kuchukua tahadhari


Amesema kuwa, kufuatia Utabiri wa Mamlaka ya Hali ya hewa Tanzania, kutakuwa na mvua kubwa zitakazonyesha kwenye mikoa mingi nchini, hivyo ni vyema wananchi wakachukua tahadhari

“Kipindi hichi cha mvua chukueni tahadha wakiwemo maderava wa vyombo vya moto ili kupunguza hasara na watu kupoteza maisha”Alisema Makonda

Pia aliwataka wananchi wanaoishi katika maeneo yenye historia ya mikondo ya maji kuchukua tahadhari kubwa kwa kuwa mvua bado zinaendelea kunyesha

Aidha, Wananchi na wafanyabiashara wenye maduka pembezoni mwa barabara hiyo wameiomba Serikali kuharakisha kukamilisha ujenzi wa Barabara hiyo ya Mianzini - Timbolo na kuomba kuangalia namna ya kuongezwa kwa vipenyo kwenye Mto Ngarenaro na daraja la Mula ili kuruhusu upitishaji wa maji mengi kwa wakati mmoja, kwa kuwa sasa madaraja hayo yanazidiwa na wingi wa maji.

Makonda, amewataka wakurugenzi wa Halmashauri zote za Mkoa wa Arusha kupitia Maofisa Mazingira na Maofisa wa Mipangomiji kufanya vikao vya dharura kwenye maeneo yao na kufanya Tathimini kwenye makazi ya wananchi ili kubaini athari zinazoweza kujitokeza endapo mvua zitaendelea kunyesha.

Maeneo aliyotembelea Mkuu wa Mkoa ni eneo la Sakina na Mianzini, maeneo ambayo yameathirika zaidi na mvua, kiasi kilichosababisha vifo vya watu 6 na uharibifu wa mali na miundombinu hususani ya barabara.