KATAVI: Mbunge wa Jimbo la Kavuu katika Halmashauri ya Mpimbwe na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Geophrey Pinda amekagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mlele mkoani Katavi.

Pinda amefanya ukaguzi wa jengo hilo Aprili 10, 2024 akiwa njiani kielekea jimboni kwake Kavuu Halmashauri ya Mpimbwe Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi kusheherekea Siku Kuu ya Eid El Fitri na waumini wa dini ya kiislamu katika jimbo lake sambamba na kukagua shughuli za maendeleo.

Pinda akiambatana na Mkuu wa Wilaya ya Mlele Alhaji Majid Mjengwa ameoneshwa kuridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo la CCM ambalo mbali na ofisi, litakuwa na ukumbi wa mikutano.

“Niwapongeze kwa kazi nzuri, naona jengo limefikia katika hatua nzuri na muda si mrefu wilaya yetu itakuwa na jengo lake zuri, hongereni sana” amesema Pinda.

Kwa mujibu wa Mbunge wa Jimbo la Kavuu, ujenzi wa jengo hilo la CCM Wilaya ya Mlele ni juhudi binafsi za yeye pamoja na mbunge mwenzake wa jimbo la Mlele Mhandisi Isack Kamwelwe.

Amesema, kukamilika kwa jengo hilo kutawawezesha watendaji wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Mlele kuwa na ofisi nzuri na hivyo kufanya kazi zao kwa ufanisi.

Akiwa jimboni kwake , Pinda mbali na kujumuika na waumini wa dini ya kiislamu katika kusheherekea Siku Kuu ya Eid El Fitri na kukagua shughuli za maendeleo katika jimbo lake pia atashiriki ziara ya Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Balozi Dk Emanuel Nchimbi anayetarajiwa kufanya ziara Mkoa wa Katavi mwishoni mwa wiki.