DAR ES SALAAM: MKURUGENZI Mkuu wa Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti na Uendeshaji wa Kilimo cha mboga za asili za majani, Kurugenzi ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, Dk Gabriel Rugalema amesema Afrika haina wataalamu wa kutosha uzalishaji mbegu hivyo inahitaji wataalamu zaidi kutoka nje.

Kutokana na hali hiyo ya ufinyu wa wataalamu Afrika, Shirika la World Vegetable Center limeamua kuanzisha mafunzo maalumu ya namna ya kuzalisha wataalamu na kwa kuanza wameanza na Shirika la NARO nchini Uganda ambapo wamekuja kujifunza namna ya uzalishaji wa mbegu za mbogamboga na matunda na huenda baada ya mafunzo hayo wakapata wataalamu zaidi.

Dk Rugalema amesema kuwa nchi nyingi za Afrika, wataalamu wa uzalishaji wa mbegu za mboga mboga ni wachache na uchache huo unalifanya Bara la Afrika kuwa tegemezi wa mbegu kutoka nje hivyo ni lazima jitihada za ziada zifanyike kupata wataalamu.

Kutokana na changamoto hiyo Serikali ya Uganda imeamua pamoja na mazao mengine wanataka kuwekeza nguvu kwenye uzalishaji wa mbegu mpya na Bora katika mazao ya mbogamboga na kuhakikisha wataalamu wao wanakuwa na utaalamu wa kina.

Dk Rugalema amesema ushirikiano ukidumishwa vizuri utasaidia kubadilishana uzoefu, elimu, mawazo na kushauriana namna ya kukatatua changamoto pindi zinapojitokeza

Naye Ofisa Mfawidhi TOSCI Kanda ya Kaskazini Dk Munguatosha Ngomuo amesema nxhu ya Uganda Sekta ya mbogamboga na matunda hasa mbegu ipo chini kutokana na sheria na kanuni zinazowawezesha kuthibiti ubora na uingizaji na uagizaji wa mbegu za mbogamboga na matunda.

Sambamba na hilo Ngomuo ameeleza ujio wa washiriki hao ni kujengewa uwezo kwani mpaka Sasa hawana “breeds program” ya mbogamboga na matunda ambayo inawawezesha wao kuanza udhibiti wa ubora wa mbegu nchini Uganda.

Kwa upande wake Ofisa Mkuu wa utafiti Kutoka Shirika la NARO, Uganda Dk Gabriel Ddamulira amesema wamekuja Tanzania kujifunza hasa katika eneo la uzalishaji wa mbegu kwani kwa wao kama nchi wanaagiza mbegu kutoka nje,sambamba na hilo ni kupata uzoefu wa uzalishaji wa mbegu kutoka World vegetable Centre.