JESHI la Polisi mkoani Kigoma limemtia mbaroni Ramadhani Shaban,21, mkazi wa Buronge Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa tuhuma za kutoa taarifa za uongo kwa wazazi wake kwamba ametekwa ili kuwezesha ndugu zake kutoa fedha kwa watekaji aweze kukombolewa.

Akizungumza na waandishi wa habari mkoani Kigoma, Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Filemon Makungu amesema kuwa mtu huyo alitoa taarifa za uongo kwa wazazi wake kwamba ametekwa ili kujipatia fedha.

Sambamba na mtuhumiwa huyo polisi pia inawashikilia watu wawili Kassimu Kibona na Ramadhani  Issa ambapo mtu huyo alikuwa akishirikiana nao kujificha (kujiteka) hadi fedha kiasi cha Sh milioni 2.5 ili waweze kumkomboa.

SOMA: Timu 16 kushiriki kombe la polisi jamii Kigoma

Kamanda huyo wa Polisi Mkoa Kigoma alisema kuwa wakati polisi wakiendelea na upelelezi Ramadhani alifikishwa na wazazi wake kituo kikuu cha polisi Mkoa Kigoma wakieleza kuwa amepatikana eneo la Msimba Dampo nje kidogo ya Manispaa ya Kigoma Ujiji baada ya kutoa fedha kwa watekaji.

Polisi imeeleza kuwa uchunguzi wa kina walioufanya umegundua kuwa watuhumiwa walitoa taarifa za uongo kwa nia ya kujipatia fedha  na hivyo kuwatia mbaroni ambapo wanatarajia kufikishwa mahakamani upelelezi utakapokamilika.