INDONESIA : RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amelipongeza na kulishukuru Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Indonesia (Indonesian Aid) kwa ufadhili wa programu mbalimbali za kuwajengea uwezo Watanzania katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Rais Dk. Mwinyi amekutana na Bw. Tormarbulang Tobing Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo pembezoni mwa Mkutano wa Pili wa Jukwaa la Indonesia na Afrika katika hoteli ya Mulia, Bali Indonesia.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi amemfahamisha Bw. Tormarbulang kuhusu dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kushirikiana na Shirika hilo katika utekelezaji wa programu mbalimbali zenye manufaa na tija kwa wananchi wa Zanzibar na kumshawishi kwa  kuangalia uwezekano wa kufadhili programu za kuwajengea uwezo walengwa.