Kabila ameahidi kuwa kurejea nchini kutatua mgogoro wa nchi

Rais wa zamani wa Jamuhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) Joseph Kabila amemlaumu mrithi wake Rais Felix Tschisekedi kwa kuiingiza nchi katika machafuko na kutoa wito kwa Wakongo kuungana ili kurejesha sheria na utulivu nchini mwao.

Bwn Kabila ameshambulia mfumo wa haki wa nchi hiyo baada ya Seneti kupiga kura ya kuondoa kinga yake, na kumfungulia njia ya kushtakiwa kwa madai ya uhaini na uhalifu wa kivita.

Kabila alitoa hotuba ya moja kwa moja kutoka eneo lisilojulikana siku ya Ijumaa, siku moja baada ya kupoteza kinga yake kwa madai ya uhusiano na kundi la M23, amesema kwamba mfumo wa haki ulikuwa "chombo cha ukandamizaji kwa udikteta unaojaribu sana kuendelea kuwa mamlakani".

Kabila mwenye umri wa miaka 53, ambaye anakanusha kuwaunga mkono waasi wanaoungwa wa M23 ambao wameiteka miji miwili mikubwa mashariki mwa nchi hiyo iliyokumbwa na mizozo, amekuwa uhamishoni tangu 2023.

Rais huyo wa zamani, ambaye amesema mara kwa mara kuwa anarejea kutoka uhamishoni kusaidia kupata suluhisho la mgogoro huo, aliishutumu Kinshasa kwa kuchukua "maamuzi ya kuudhi kwa mzaha".

‘’Nimeamua kuvunja ukimya, kwa sababu kwa kuzingatia hali ambayo nchi yetu inapitia, kuendelea kukaa kimya kungenifanya nifunguliwe mashtaka mbele ya mahakama ya historia, kwa kushindwa kusaidia zaidi ya watu milioni mia moja walio hatarini’’, alisema Kabila.

Seneti ya DRCilipiga kura kwa wingi Alhamisi kukubali ombi la serikali la kuondoa kinga ya maisha ambayo Kabila kiongozi wa nchi hiyo kutoka 2001 hadi 2019 – alikuwanayo kwasababu ya cheo chake cha heshima kama "seneta wa maisha".

Waziri wa Sheria Constant Mutamba alisema uhalifu unaodaiwa na Kabila ni pamoja na "uhaini, uhalifu wa kivita, uhalifu dhidi ya ubinadamu na kushiriki katika vuguvugu la uasi" mashariki mwa nchi.

Siku ya Ijumaa, Kabila alisema uhuru wa DRC na uadilifu wa eneo hauwezi kujadiliwa. "Kama mwanajeshi, niliapa kutetea nchi yangu ... Ninabaki kuwa mwaminifu zaidi kuliko hapo awali kwa kiapo hiki," alisema.

Kurudi kwa Kabila nchini DRC kunaweza kutatiza juhudi za kumaliza uasi mashariki, ambayo ina usambazaji mkubwa wa madini muhimu ambayo utawala wa Rais wa Marekani Donald Trump una hamu ya kufikia.

Washington inashinikiza makubaliano ya amani kutiwa saini kati ya DRC na Rwanda msimu huu wa kiangazi, yakiambatana na mikataba ya madini inayolenga kuleta mabilioni ya dola za uwekezaji wa Magharibi katika eneo hilo, kulingana na Massad Boulos, mshauri mkuu wa Trump kwa Afrika, aliyenukuliwa na shirika la habari la Reuters.