GEITA: TANZANIA imefanikiwa kusajili jumla ya miradi 1,828 ya uwekezaji yenye thamani ya Dola za Kimarekani bilioni 20.31 sawa na Sh trilioni 50.37 kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2024 hadi 2025.
 
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Balozi Dk Aziz Mlima ametoa taarifa hiyo akiwa ziarani mkoani Geita.
 
Dk Mlima amesema hatua hiyo imesaidia upatikanaji wa ajira zipatazo 375,188 ikiwa ni matokeo ya kitaifa ya uhamasishaji uwekezaji wa ndani.
 
Amesema mwaka 2024 mamlaka ilisajili miradi 901 Yenye thamani ya Zaidi ya Dola za Marekani bilioni 9.31 na kutoa ajira zaidi ya 212,293 huku kukiwa na mwitiko mkubwa wa wazawa.

Amesema kwa mwaka 2024 miradi ya watanzania imeendelea kuongezeka maradufu ambapo jumla ya miradi 497 inamilikiwa na Watanzania sawa na asilimia 55 ya miradi iliyosajiliwa.

“Mwaka 2025 ilisajiliwa jumla ya miradi 927 yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 11 na kutoa ajira zaidi ya 162,895 ikiwemo miradi 469 inamilikiwa na watanzania sawa na asilimia 51”.

Amesema ili kuongeza mwamako, TISEZA imetenga siku 82 za kampeni ya Kitaifa ya Uhamasishaji Uwekezaji wa Ndani kuanzia Januari 18, 2026 hadi Aprili 09, 2026 katika Mikoa yote ya Tanzania

Amesema Kupitia kampeni hiyo, Mamlaka ya Uwekezaji Nchini inatarajia kuongeza idadi ya Miradi ya Uwekezaji wa ndani katika skimu ya kawaida na Skimu Maalum mara dufu.

Mkuu wa mkoa wa Geita, Martine Shigela amesema elimu endelevu inahitajika kwa wazawa ili wafanye uwekezaji wao katika mfumo rasmi na kuchangia katika pato la taifa na kutoa ajira.

Amesema mkoa wa Geita umejizatiti kuendelea kuanika fursa za kiuchumi kupitia sekta zote ikiwemo uvuvi, ufugaji, kilimo, viwanda na biashara ili kufikia azma ya uwekezaji wenye tija.

“Kama mkoa tumeshakubaliana kuhakikisha kwamba hakuna sekta inayolala, ili siyo kila mtu afikirie Kwenda kufanya uchimbaji wa madini”.