Burkina Faso imekataa ripoti iliyosema zaidi ya raia 1,800 wameuawa katika vitendo vinavyofikia "uhalifu dhidi ya ubinadamu" katika kipindi miaka mitatu tangu Ibrahim Traoré achukue madaraka.

Serikali siku ya Jumapili iliita ripoti ya Human Rights Watch (HRW) kuwa "ya uwongo", ikipuuza matokeo hayo kama "uvumi na madai makubwa yasiyo na msingi".

Ripoti hiyo ina "kusudi moja tu ... kuwadhalilisha" wanajeshi wa nchi hiyo, ambao wamekuwa wakipigana kwa "utaalamu," taarifa yake iliongeza.

Serikali imekana shutuma za awali kwamba vikosi vyao vimewaua raia. Wiki iliyopita, HRW ilihusisha mauaji mengi, 1,255 na wanajeshi na wanamgambo washirika.

Kundi la kutetea haki za binadamu liliwashutumu wanamgambo wa Kiislamu waliobaki.

Takribani raia 1,837 waliuawa katika matukio 57 kati ya Januari 2023 na Agosti 2025, wakiwemo watoto kadhaa, ripoti hiyo ilisema.

HRW iligundua kuwa Rais Traoré na makamanda sita wakuu wa jeshi "wanaweza kuwajibika kwa dhuluma kubwa na wanapaswa kuchunguzwa".

Pia ilisema viongozi watano wa jihadi wanaweza kuwa na hatia.

Moja ya sababu ambazo jeshi lilitoa kwa kunyakua madaraka ilikuwa ni kukabiliana na makundi ya jihadi yenye uhusiano na al-Qaeda ambayo yamekuwa yakifanya uasi nchini Burkina Faso na nchi jirani kwa zaidi ya muongo mmoja na kudhibiti sehemu kubwa za nchi.