DAR ES SALAAM: Rais wa Kenya, William Ruto amewasili Tanzania leo Mei 4, 2026 kwa ziara ya kitaifa ya siku mbili inayolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya.
 
Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu Tanzania, Ruto atafanya mazungumzo ya ana kwa ana na mwenyeji wake, Samia Suluhu Hassan, kabla ya mazungumzo rasmi ya ujumbe wa nchi zote mbili.
 
Mazungumzo hayo yataangazia sekta za biashara, uwekezaji, miundombinu na usafirishaji, huku viongozi hao wakitarajiwa pia kushuhudia utiaji saini wa mikataba ya ushirikiano.
 
Aidha, Rais Ruto atashiriki Jukwaa la Biashara litakalowakutanisha wafanyabiashara na wawekezaji wa Tanzania na Kenya, na kuhutubia Bunge jijini Dodoma Mei 5, 2026 kabla ya kuhitimisha ziara yake.
 
Ziara hiyo inaakisi kuimarika kwa mahusiano ya kiuchumi na kidiplomasia kati ya mataifa hayo jirani.