KAMATI ya Kudumu ya Bunge Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imempongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kwa ujenzi wa shule za kisasa za ghorofa wilayani Ilala na kueleza kwa mara ya kwanza kamat hiyo imeshuhudia jengo la shule ya sekondari ya kata yenye lifti.
Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo Florent Kyombo, katika ziara ya wajumbe wa kamati hiyo kukagua miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaa, hususan ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Bonyokwa itakayo chukua wanafunzi wa kidato cha tano na sita.
Kyombo amesema kamati yake imezunguka mikoa mingi Tanzania lakini haijawahi kukutana na jengo la shule lenye hadhi kama hilo la Shule ya Sekondari Bonyokwa lenye lifti.
"Jiji la Dar es Salaam wameupiga mwingi. Msione vinaelea viumeundwa. Tumezunguka mikoa mingi lakini hatujakutana na jengo lenye hadhi kama hii,"ameeleza Mbunge Kyombo.
Amesema kamati hiyo inamshukuru Rais Dk. Samia, kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya elimu hususan ujenzi wa shule za ghorofa ambao utaondoa adha kwa wanafunzi.
"Kamati inawaomba wanafunzi kumlipa Rais Dk. Samia, kwa kufanya vizuri darasani na kutunza mundombinu hii,"amebainisha Kyombo.
Ameongeza licha ya kutembelea na kukagua jengo hilo la shule lakini maelezo ya awali ya viongozi wa wilaya ya Ilala na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam yanadhihirisha ujenzi wa majengo mengi ya ghorofa hivyo kupongeza viongozi kwa utekelezaji wa miradi hiyo .
Hata hivyo kamati hiyo ilielekeza halmashauri hiyo kuboresha majengo ya Shule ya Msingi Bonyokwa na Shule ya Sekondari Bonyokwa ya kiadato cha kwanza na cha nne, yawiane kidogo na hadhi ya jengo hilo la kissa.
Mbali na mradi huo, kamati hiyo mekagua ujenzi wa Barabara ya Kwa mpalange (Buza) Temeke-Kitunda unaogharimu kilometa 6.2, ujenzi wa Kituo cha Afya Mchikichini unaotekelezwa katika Kata ya Mchikichini unaogharimu sh. bilioni 7.4.
Awali Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, alimshukuru Rais Dk. Samia, kwa kuelekeza fedha nyingi za miradi wilayani humo na kwamba wataendelea kusimamia kikamilifu kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati
Mpogolo, ameeleza ujenzi wa shule za ghorofa ni mkakati uliwekwa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kusimamia maono ya Rais Dk. Samia, wanafunzi wanasoma katika mazingira rafiki.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam,Elihuruma Mabelya, amesema katika mwaka wa fedha 2026-27 wametenga sh. bilioni 19 kuboresha mundombinu ya elimu.
Mabelya amesema mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari Bonyokwa umegharimu sh. bilioni 2.07 na ina madarasa 20, matundu ya vyoo 45 yakijumuisha matundu ya vyoo vya kawaida 30, matundu ya watu wennye mahitaji maalum 10, sehemu za kujisaidia haja ndogo tano kwa wavulana, vyumba vitano maaluma kwa wasichana vyenye choo ndani yake
"Shule hii inatarajia kuchukua wanafunzi 1400 mwaka 2026/27 na mwaka mwaka 2028 shule itachukua wanafunzi 3100,"amesema Mabelya.
Mbali na jengo la Shule ya Sekondari Bonyokwa kuwa na lifti shule nyingine ambayo jengo lake lina lifti wilayani humo ni Shule ya Sekondari Kipunguni B.






0 Comments