Waziri Mkuu wa Israel aagiza mashambulizi Beirut wakati mvutano na Hezbollah ukiendelea kuongezeka

Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, ameagiza mashambulizi kufanywa katika vitongoji vya kusini mwa mji mkuu wa Beirut, huku mapigano kati ya Israel na kundi la Hezbollah linaloungwa mkono na Iran yakiendelea kuongezeka.

Netanyahu alisema kuwa maeneo aliyoyataja kama "maeneo ya kigaidi" katika eneo la Dahieh, ambalo ni ngome ya Hezbollah, yatalengwa kwa mashambulizi.

Alidai hatua hiyo ni jibu kwa mashambulizi dhidi ya raia wa Israel na ukiukwaji mwingine wa makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyosimamiwa na Marekani mwezi Aprili, lakini ambayo yameshindwa kumaliza mapigano.

Afisa mmoja mwandamizi wa serikali ya Lebanon aliliambia shirika la habari la BBC kuwa serikali yake inategemea juhudi za upatanishi za Marekani kushinikiza Israel kusitisha ukiukwaji wake wa makubaliano hayo na kuzuia vifo zaidi vya raia.

Siku ya Jumapili, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, alizungumza kwa simu na Netanyahu pamoja na Rais wa Lebanon, Joseph Aoun.

Kwa mujibu wa afisa mmoja wa Marekani, Rubio alisema kuwa kama hatua ya kwanza, viongozi wa Lebanon waishinikize Hezbollah kusitisha mashambulizi yake dhidi ya Israel. Kwa upande mwingine, Israel itaepuka kuongeza mashambulizi Beirut.

Afisa huyo alisema hatua hiyo inaweza kutoa nafasi ya kupunguza mvutano hatua kwa hatua na kufanikisha kusitishwa kwa mapigano.

Wakati huo huo, wanajeshi wa Israel walioko kusini mwa Lebanon walivuka Mto Litani na kuteka Beaufort Castle, ngome yenye historia ya zaidi ya miaka 900 iliyopo kwenye eneo lenye umuhimu mkubwa wa kijeshi.

Waziri wa Ulinzi wa Israel, Israel Katz, alisema operesheni yao "bado haijaisha" na kwamba wana azma ya kudhoofisha na kuvunja nguvu za Hezbollah.