IRINGA: BIASHARA za barabarani zimeibua kilio kwa wafanyabiashara wa Soko Kuu la Iringa, waliotaka Serikali kurejesha utaratibu kwa kuwaondoa wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao pembezoni mwa barabara.

Wakizungumza katika mkutano wa Kata ya Kitanzini uliofanyika katika Soko Kuu la Iringa, wafanyabiashara hao walisema soko hilo ni kitovu cha biashara na linahitaji kuwekewa mazingira yatakayowawezesha kufanya shughuli zao katika maeneo rasmi.

Mfanyabiashara wa soko hilo, Godfrey Mhanga, alisema biashara zinazofanyika nje ya soko zimekuwa zikisababisha msongamano na kuathiri matumizi ya barabara, hivyo akaitaka Serikali kutekeleza agizo la kuwahamisha wafanyabiashara hao kwenda katika maeneo rasmi.

Mhanga pia alimtaka Mbunge wa Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo, kuwa sauti ya wananchi Bungeni bila kujali masuala ya kisiasa.

“Ukifika Bungeni sahau UCCM wako, wakilisha wananchi,” alisema. Katika mkutano huo, Ngajilo alitoa TV mbili mpya kwa ajili ya Soko Kuu la Iringa, ikiwa ni sehemu ya kuchangia kuboresha mazingira ya soko hilo.