Kumetokea mripuko mkubwa katika kinu cha nuklia cha Japan, ambacho kiliharibika katika tetemeko kubwa la ardhi la jana.Waziri Mkuu amewasihi walio karibu na kinu hicho cha Fukushima kuhama.
Kuta za chuma tu za kinu hicho ndio bado zimesimama. Wafanyakazi wane wamejeruhiwa.
Msemaji wa serikali alieleza kuwa uchunguzi bado unafanywa juu ya mripuko wa kinu hicho, kilioko kilomita miambili na hamsini kaskazini mwa Tokyo.
Kulingana na habari za awali, televisheni nchini Japan, imeonesha magari, meli na hata majengo makubwa yakizolewa na mawimbi makubwa ya maji ya bahari baada ya tetemeko lenye ukubwa wa 8.9 kupiga.
Tetemeko hilo pia limesababisha moto
katika maeneo mengi ya Japan ikiwemo mji mkuu Tokyo, ambapo imearifiwa watu 15 wamekufa.
Limepiga kiasi cha kilometa 400 kutoka mji mkuu na mawimbi yakaingia umbali wa maili 20 ndani.
Wataalam wa matetemeko wamesema hili ni moja ya tetemeko kubwa kuipiga Japan kwa miaka mingi.
Wakati tetemeko lilipopiga, majengo mjini Tokyo yaliyumba. Mtu kutembea ilikuwa sawa na kuwemo ndani ya meli inayopigwa mawimbi baharini.
Watu walishuka chini kutoka katika ofisi zao na kusalia mitaani wakiwa wanatetemeka.
Moto mkubwa ulizuka katika eneo moja la mji na katika maeneo mengine, watu waliojeruhiwa walitolewa nje ya vituo.
Mara moja serikali ilitoa onyo la tsunami.
Katika mji mkuu Tokyo, usafiri wa umma umesimamishwa, lifti katika majengo mengi zimezimwa na maelfu ya watu wamekusanyika katika bustani za wazi na vituo vya treni.
Onyo la tsunami limetolewa pia katika maeneo yote ya bahari ya Pacific ikiwemo Philippines, Indonesia, Taiwan, Hawaii, na mwambao wa bahari ya Pacific nchini Urusi na kaskazini mwa Amerika Kusini.
Mawimbi makubwa yalipiga katika miji ya Miyagi na Fukushima, na kuharibu vibaya sehemu kubwa ya makazi ya watu eneo la pwani. Shirika la habari la Kyodo limesema mawimbi yaliyofikia urefu wa mita 10 na kupiga bandari ya Sendai huko Miyagi .
                                Magangaone.blogspot.com