Waziri Mkuu wa Italia, Silvio Berlusconi,(pichani) amethibitisha kwamba atajiuzulu wadhifa huo.
Hata hivyo, amesema hataondoka hadi pale bunge litakapoidhinisha mpango wa marekebisho ya kufufua uchumi wa nchi hiyo.
Uchumi wa Italia umeathirika vibaya kutokana na mzozo wa madeni unaokumba mataifa yanayotumia sarafu ya Euro.
Mapendekezo hayo yatawasilishwa bungeni katika wiki mbili zijazo.
Bwana Berlusconi alitangaza mpango wa kujiuzulu baada ya kura iliyobainisha kuwa umaarufu wake bungeni umepungua.
Kiwango cha riba katika hawala ya serikali ya Italia ilishuka Jumatano iliyopita, kumaanisha kuwa sasa bei za hawala hizo zimeshuka kwa nchi hiyo kukopa kutoka kwa masoko ya kifedha.
Kulikuwa na fununu kuwa iwapo Bwana Berlusconi angejiuzulu, utawala ambao ungechukua nafasi hiyo ungeundwa na kundi la watalaam, ambao jukumu lao kuu lingekuwa ni kuinua uchumi wa nchi hiyo.
Lakini bwana Berlusconi amepinga hilo. Amesema kwa maoni yake,'' kufanyika kwa uchaguzi ndio njia pekee ya nchi hiyo kupiga hatua''.
Bwana Berlusconi ametawala siasa za Italia kwa kipindi cha miaka 17.
Ameponea kura 50 za kutokuwa na imani naye, lakini hivi karibuni amezongwa na misururu ya sakata za kisheria na ngono, pamoja na migororo ya kisiasa na kiuchumi.