DEREVA wa pikipiki za kukodi maarufu kama 'bodaboda', Mussa Kimbei (43), ameuawa kikatili kwa kucharangwa mapanga na wananchi baada ya kufumaniwa akifanya mapenzi na mke mdogo wa mfanyakazi wake.

Inadaiwa kuwa marehemu ambaye ni mkazi wa eneo la Kichangani mjini Mpanda alikuwa pia akimiliki shamba la tumbaku ekari nane na ekari nne za shamba la mahindi katika Kijiji cha Kambanga ambapo aliajiri walinzi na vibarua wanane.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Rukwa, Isuto Mantage, mauaji hayo yalitokea
juzi saa tano usiku shambani kwa marehemu katika kitongoji hicho cha Kambanga baada ya
kufumaniwa akifanya mapenzi na mke wa msimamizi wa shamba lake aitwaye Christopher
Bonge.

Mantage alisema mbali ya kumuua kikatili kwa kumcharanga vipande vipande kichwa kwa
mapanga, wananchi hao walichoma moto vibanda vitatu vya kukaushia tumbaku na kufyeka
mashamba yake ya tumbaku na mahindi kisha wakateketeza pikipiki yake kwa moto.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwa masharti ya majina yao kutoandikwa gazetini, baadhi
ya madereva wa bodaboda ambao wanadai kuwa marafiki wa karibu wa Kimbei, wanadai kwa muda mrefu Kimbei alikuwa akituhumiwa kufanya mapenzi na wake za wanakijiji hao wa Kambaga.



“Kimbei ambaye ameacha wake wawili na watoto tisa, inadaiwa alikuwa akitumia fedha zake baada ya mauzo ya tumbaku kurubuni wake za wanakijiji hao. Huyu mke mdogo wa msimamizi wa shamba lake walikuwa na uhusiano wa kimapenzi wa muda mrefu,” alisema mmoja wa madereva hao.

Habari zaidi zilisema Kimbei alikuwa akirudi mjini Mpanda amalizapo kukagua shamba lake, lakini kwa kutumia pikipiki alikuwa akienda kijijini Kambaga usiku na kukutana na 'wapenzi' wake hao ambao inadaiwa ni wake za watu.

Kwa mujibu wa Kamanda Mantage usiku huo wa tukio wananchi zaidi ya 20 walikwenda
nyumbani kwa Christopher kijijini hapo, ambapo walimweleza kuwa mkewe mdogo na Kimbei walikuwa kibandani shambani wakifanya mapenzi.

Alisema inadaiwa taarifa hiyo ilimshitua sana na kumghadhabisha Christopher ambaye
alikubali kufuatana na wanakijiji wenzake hadi shambani kwa Kimbei wakiwa wamebeba silaha
za jadi yakiwamo mapanga na marungu.

Kamanda Mantage alisema baada ya kufika shambani walimfumania Kimbei akifanya mapenzi na mke wa Christopher, akiwa uchi na walimshambulia na kukicharanga kichwa na kisha kumpiga kichwani 'mpenzi' wake kwa panga hadi akazirai.
Alisema mke huyo mdogo wa Christopher alikimbizwa katika Hospitali ya Wilaya mjini hapa
kwa matibabu ambapo hali yake inasemekana bado ni mbaya.

Kwa mujibu wa Mantage muda mfupi kabla wananchi hao kuwasili shambani kwa marehemu,
walinzi na vibarua wake walikimbia na kulitelekeza shamba hilo wakihofia usalama wao.

Juzi jioni gazeti hili lilishuhudia msururu wa madereva wa 'bodaboda' zaidi ya 400 wakiendesha pikipiki hizo kusindikiza mwili wa marehemu kwenda makaburi ya shule ya msingi ya Nyerere mjini hapa kwa maziko.

Kamanda Mantage alisema Polisi inalichunguza tukio hilo la mauaji na inashikilia watu
watatu akiwamo Christopher kwa mahojiano.