WATAALAMU wanaoshughulika na hifadhi ya mazingira nchini Tanzania wamegundua
kipiribao (nyoka mwenye sumu kali) mwenye pembe ambaye wanasema yuko katika hatari ya kutoweka.

Nyoka huyo mwenye rangi za kupendeza za njano na nyeusi ameelezwa kufanana na nyoka
anayepatikana katika milima ya Usambara na hata Uluguru anayekwenda kwa jina la Usambara.

Nyoka huyo mpya ambaye makazi yake bado kuelezwa kiusahihi anapatikana katika nyanda za juu kusini mwa Tanzania na alibainika wakati wa tathmini za kibaiolojia kwa mwaka 2010 na 2011 katika maeneo hayo.

Wataalamu wanaohusika na utafiti huo wamekataa kuelezea eneo halisi wanakopatikana nyoka hao kwa hofu ya wapenzi wa wanyama kwenda kuwawinda na kuwatwaa wakati viumbe hao inaonekana wapo katika kundi la wanaotoweka duniani.

Kipiribao huyo ambaye alielezwa kwa undani katika jarida la utafiti la Zootaxa la Desemba 6,2011 anaonekana kama mwindaji wa usiku na chakula chake kikuu ni vyura ambao huwapata kandoni mwa mito.
Kwa mujibu wa maelezo nyoka huyo anafanana na kipiribao mwingine anayejulikana kama Usambara ambaye inaaminika hupatikana pia katika milima ya Uluguru.




Matilda ambaye kwa jina la kibaolojia anajulikana pia kama Atheris matildae, alipewa jina hilo kwa heshima ya binti wa Mkurugenzi wa shirika la kimataifa la hifadhi ya wanyama Tim Davenpor, ambaye pia ni mwandishi mwenza wa taarifa hiyo ya utafiti kuhusu nyoka iliyochapishwa katika jarida hilo la kimataifa.

Ukimwangalia nyoka huyo rangi za njano na nyeusi zimekosa na kuonekana waziwazi na ama hakika huna sababu ya kuhoji rangi aliyopakwa na Mungu. Nyoka huyu mpya ana urefu wa
futi 2.1 na ana pembe zilizotengenezwa kwa magamba juu ya macho yake yaliyojitokeza kama ya kinyonga.

Hakuna mtu kwa uhakika anayejua kwanini nyoka hawa wana pembe ingawa kuna watu wanabuni maelezo kwa kuzingatia mazingira ya nyoka hao walipoonekana. Lakini wengi wanakubaliana na nadharia kwamba zinahami macho au hata ya kujitambulisha miongoni
mwa nyoka wenyewe wakati wa kutafuta wapenzi.

Inawezekana kabisa kuwa pembe hizo zina kazi mbalimbali; lakini katika hilo Davenport na wenzake hawajishughulishi nalo. Wao hasa kinachowashughulisha ni uwezekano wa majangili kuwanasa nyoka hao na kuwauza kwa watu wengine na ndio maana watafiti hao mpaka sasa hawataki kusema kwa yakini wapi wanapatikana nyoka hao.

Lakini pamoja na kutosema walieleza kuwa wanapatikana katika eneo dogo na tayari limeshaharibiwa vibaya na watengeneza mkaa na wakata mbao. Davenport na wenzake
wanaamini kwamba aina hii ya nyoka itawekwa katika daraja la wanaotishia kutoweka kabisa duniani.

Pamoja na tatizo hilo wameanzisha eneo dogo kwa ajili ya kuzaliana kwa nyoka hao. Tofauti ya Matilda na Usambara labda ni katika rangi na urefu. Usambara (Atheris ceratophora) ni kipiribao anayepatikana katika safu chache za milima nchini Tanzania na ambaye hukua kufikia sentimeta 54 huku wa kike wakiwa wakubwa kuliko wa kiume.

Urefu wa kipiribao dume wa Usambara ni kama sentimeta 42 na mkia wake ni kama sentimeta nane. Rangi ya kipiribao wa Usambara ni njano inayoelekea katika ukijani na wakati mwingine akiwa na rangi ya kijivu.Tumbo lake kama rangi ya chungwa.

Pamoja na kwamba wanasema nyoka matilda anafanana na Usambara bado ana tabia zake ambazo wataalamu wanaanza kujifunza lakini wakati wanajifunza wanatafuta njia mbadala za kumwezesha kuendelea kuwapo katika eneo ambalo linaharibiwa mazingira yake kwa kasi.

Imetafsiriwa kutoka mtandaoni