Korea Kaskazini imeishutumu Korea Kusini, kuwa iliwatumia raia kama kinga, ili kulinda vituo vyake vya kijeshi, kwenye kisiwa ambacho kilishambuliwa na Korea Kaskazini, mapema hivi karibuni.
Raia wawili pamoja na wanajeshi wawili wa Korea kusini, waliuawa katika mashambulio hayo ya makombora. Kaskazini inasema, vifo vya raia vinatumiwa kama propaganda.
Mazishi yamefanywa ya wanajeshi wawili waliouwawa katika mashambulio hayo, huku Korea Kusini na Marekani, zinajitayarisha kufanya mazoezi ya majeshi ya wanamaji katika bahari ya Yellow Sea.

Korea Kaskazini imeonya mazoezi hayo, yatasababisha vita kuzuka katika Rasi ya Korea. Lakini msemaji wa mkuu wa majeshi ya Korea Kusini, Lee Bung-Woo, amesema, lengo ni kuizuwia Korea Kaskazini, isishambulie tena.