Utawala wa Kanali Muammar Gaddafi uko chini ya shinikizo kali, kufuatia maandamano makubwa katika mji mkuu wa Libya na pia kujiengua kwa baadhi ya mabalozi.Maafisa wa usalama walifyatua risasi na mabomu ya machozi kwa waandamanaji katika mitaa ya Tripoli siku ya Jumapili.
Mji wa pili kwa ukubwa, Benghazi, sasa unaonekana uko chini ya udhibiti wa waandamanaji.
Lakini mtoto wa Kanali Gaddafi, Saif al-Islam, ameonya kuwa vita vya wenyewe kwa wenyewe huenda vikazuka. Katika hotoba ndefu kupitia televisheni, ametoa mapendekezo ya mabadiliko ya kisiasa, lakini pia kuahidi kuwa utawala huo "utapigana mpaka mwisho" dhidi ya "wachochezi".

Amekiri hata hivyo kuwa miji ya mashariki ya Benghazi na al-Badya imechukuliwa na wapinzani.
Waziri wa sheria Mustapha Abdul Jalil amekuwa afisa wa hivi karibuni kujiuzulu. Amesema alikuwa akiachia madaraka yake kwa sababu ya "matumizi makubwa ya nguvu", amekaririwa na gazeti binafsi la Quryna, siku ya Jumatatu.
Siku ya Jumatatu, taarifa kutoka Tripoli zilikuwa zikisema mitaa ilikuwa kimya, huku majeshi ya serikali yakifanya doria.