Serikali ya Kenya imekariri kuwa kamwe haiwezi kuzungumza na kundi la wapiganaji la al-Shaabab.
Akiongea katika makao makuu ya wizara ya ulinzi, katibu katika wizara ya usalama wa ndani, Francis Kimemia, amesema Kenya itaimarisha mikakati yake ya kijeshi dhidi ya kundi hilo, hadi pale itapopata hakikisho thabiti la usalama wake.
Mkuu wa majeshi nchini Kenya, Jenerali Karangi, amethibitisha kuwa tangu mikakati hiyo ya kijeshi kuanza nchini Somalia, mwanajeshi wake mmoja ameuwawa na watatu wametoweka, huku kuna wasi wasi, kuwa huenda wametekwa na wapiganaji wa al Shabaab.
Piya alisema wanajeshi watano wamejeruhiwa huku mmoja alifariki kutokana na majaraha aliyopata, baada ya jeshi la Kenya kushambuliwa na al-Shabaab..

Amekariri kuwa Kenya haina nia yoyote ya kunyakuwa ardhi ya Somalia, ila lengo lake kuu ni kuimarisha usalama wake kufuatana na sheria za kimataifa.
Piya inaarifiwa kuwa mapigano makali yametokea katika kambi ya wanajeshi ya Umoja wa Afrika mjini Mogadishu, ambako wapiganaji wa al-Shabaab walifanya mashambulio mawili ya kujitolea mhanga.