KIZAZI kijacho huenda kisijue nini hasa maana ya Bagamoyo, mji uliokuwa na barabara ya kwanza ya uhakika, mji wa kwanza makao makuu ya koloni la Kijerumani na bandari ya kwanza kusafirisha pembe za ndovu na watu kama bidhaa.

Kwa wale wanaopenda kuujua mji wa Bagamoyo katika mkoa wa Pwani, wataujua kwa namna ambavyo wao wanapenda kuujua. Lakini, kwa wanazuoni na watafiti wa masuala ya jamii na historia yao, ni dhahiri mji huu unatoweka katika mazingira yao kwa spidi ya mwanga, ingawa wenyeji hawalioni hilo.

Nilipata bahati ya kwenda Bagamoyo hivi karibuni. Nilifikishwa na waungwana pale kwenye Msalaba, lakini niliporudi katika nyumba niliyofikia, niliwafikiria wote wanauzuru Bagamoyo.

Naam, wanaozuru Bagamoyo wawe wale wa kidini, kihistoria au kwa burudani, kitu kimoja kiwazi kabisa Bagamoyo mji wenye fursa na changamoto za kimaendeleo, unakuwa mji wa kisasa, ukizima historia iliyopo polepole, na mimi nathubutu kusema unakufa kihistoria,
wakazi wake hawana cha kujivunia.



Huhitaji tafakari kubwa ya kiprofesa, kujua kwamba hata katika Mji wa Wafu, Kaole, uchakavu wake si wa kawaida na hata kama kunaonekana dalili za kuhifadhiwa, upo ukweli kwamba hili ni tatizo.
Kizazi cha sasa hakiangalii sana uzima wa ukuukuu, unaostahili kuwapo katika mji, ambao unakuwa bandari, unakuwa mji wa kufikia, unakuwa mji wa pilikapilika za kisasa zaidi.

Mji huu wa zamani nchini Tanzania, wenye haiba ya aina yake kihistoria, unakwenda pamoja na nyaraka nyingi kuonesha kwamba zipo juhudi za kuhifadhi mji huo, ambao zamani ulikuwa maarufu kama kituo cha biashara na mji wa kwanza wa watawala wa Kijerumani.

Ukitaka kujua kwamba mji huu wa kihistoria unakufa ndani ya historia, maana ya Bagamoyo inateleza katika mdomo tu, lakini maboma yale pasi shaka yanatoweka na vidatu vya kuingilia baharini, pia zinatoweka na alama za njia, pia zinatoweka na mabaki ya maboma pia yanatoweka.

Ruksa za ujenzi hazizingatii historia, inayoonesha kuwa Bagamoyo kilikuwa kituo kikuu cha kibiashara, japokuwa biashara ya watu kama bidhaa ilikomeshwa duniani mwaka 1873 na kuendelea karne yote ya 19, kwamba wamisironari wa kwanza walifika hapo na kuchomeka msalaba, eneo ambalo linabanwa na mahoteli na kwamba wajerumani walitengeneza boma lao la kwanza la kiutawala pale.
Majani yanayoota hovyo, hayaoneshi uzuri wa historia na maswali kuwa kisima cha kwanza
kilikuwa wapi, si rahisi kujibika. Usasa? Bagamoyo ambao upo kilomita takribani 65 kutoka Dar es Salaam katika mazingira ya kawaida, si mbali vya kutosha kutofanya maisha ya starehe kwa wakazi wake.

Lakini, pamoja na umbali huo hafifu wa Bagamoyo inaonekana kuchakaa kwa kasi na kuchusha, si kwa umaridadi wa sasa, bali kukosekana kwa ukarabati wa majengo ya zamani na miundombinu ya zamani kuweka historia kama zamani.

Nuru ya maendeleo ya kisasa kwa wakazi wanaoonekana kuwa na shida zaidi pengine kuliko ukubwa wa mji na jina lao, Bagamoyo imekosa mvuto wa kihistoria kwa wananchi wake na majengo yaliyobaki kuelezea Bagamoyo haitoshi kufikisha ujumbe stahiki kwa mji wa Kwanza ulionakshiwa na historia ya Waarabu, Wajerumani na wamisionari.

Bagamoyo jina kubwa tangu wakati wa utawala wa kiarabu, utawala wa Kijerumani na hata kwa
waingereza, sasa umeongezwa umaarufu zaidi kwa kuwa Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete, anatoka katika mji huo, lakini hata kwa wale wanaotengeneza zana za sanaa pale penye picha nyingi za watu maarufu, unaweza kujiuliza inawezekana kwa muda gani!

Utajiri mkubwa unaostahili Bagamoyo wa utalii - uwe wa ndani au nje, haujaonesha kama utaweza kuwapo kwa miaka mingi ijayo na kusaidia wananchi wa hapa, ambao ama hakika walistahili kujivuna.

Fikira za sekta ya utalii kumeremetesha historia ya wenyeji wa Bagamoyo, zinazongwa na
ujenzi wa mahoteli ambao kwa namna ya tafakari ya karibu, yanachukua usasa zaidi na kuendekeza utalii wa kwenye fukwe kuliko kusoma historia na makazi ya zamani.
Kwa Adamu Mponda (29) ambaye pia ni mkazi wa Bagamoyo, mabadiliko yanayotokea,
yanaongeza shida zaidi badala ya kupata njia ya kutanzua yaliyopo, kwa kuelimisha maana ya kutunza kila kitu kilichokuwapo hapo kale kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

Mawazo ya kuwapo kwa utalii, yamewezesha kuwapo kwa ujenzi wa mahoteli, lakini mahoteli hayo yanasaidia nini katika hifadhi ya jina na mambo yanayogusa Bagamoyo?

Viwanda vingi vinafikiriwa, maeneo ambayo ni ya wenyeji na yenye historia za aina yake, nayo yanauzwa na wenyeji hao na hakuonekani kama kuna juhudi zozote zile za kuhifadhi maeneo, si tu ya wakoloni, lakini hata yale ya tambiko.

Ukiuliza maswali ni bajeti kiasi gani, inatengwa kuhifadhi na kununua maeneo yanayostahili kuhifadhi ili kusiwepo na uharibifu wa kihistoria, kama majengo yanavyovunjwa Dar es Salaam kwa neno la usasa na kuondoa hatari kwa maisha ya wakazi wa majengo hayo,
Bagamoyo nako vivyo hivyo.

Wakati wenzetu wazungu, hupiga picha majengo hayo na kumwelekeza mtu ajenge kwa namna
ile ile, lililopokuwapo jengo, sisi tunafuta historia kabisa. Je, watu zamani kabla ya kuendelea
na safari walikula nini, mashamba yao yalikuwa wapi? Leo ukiuliza, huwezi kupata hata hilo jibu la njia za mzunguko za kufikia bandarini kutoka kwenye boma na soko.

Pamoja na ukweli kuwa Bagamoyo haineemeki na kuwa historia ya kuwa makao makuu ya Ujerumani, kituo cha biashara enzi za watumwa na mipango miji ya kwanza kwa Tanganyika, Bagamoyo haionekani kuwa na mipango endelevu ya kutunza rasilimali, ambayo ni mbegu ya utajiri wa elimu wa tabia za wananchi na athari za biashara za watu katika mji huo.
Pamoja na fukwe nzuri, Bagamoyo ni eneo muhimu kwa kitamaduni, pwani na kitovu cha makutano wa kitalii kwa pwani ya Tanzania. Ni dhahiri kuna changamoto za kijamii katika kutunza uasili wa mji wa Bagamoyo, changamoto ambazo baadaye zitanyima hata hao watalii
kidogo, wanaofika sasa kufuatilia mambo mbalimbali.

Kama vile kuleta watalii bila kubadilisha utamaduni na kutumia sekta kwa ajili ya maendeleo ni kitu kisichoonekana.

Watu kama Yusufu (22) ambaye ni machinga katika eneo Msalabani, akiwa anauza kazi za mikono (sanaa), wana wasiwasi kuhusu kesho, kwa sababu wanunuzi wengi wa kazi hizo ni wazungu (watalii), ambao katika mazingira ya sasa ya kutohifadhiwa kwa mji, kuwezesha utalii wa kale na yeye hatakuwa na kitu cha kuuza.

Ras T ambaye anamiliki studio kwa ajili ya sanaa, akitoa maoni yake, anasema anadhani serikali imeshindwa namna ya kuusaidia umma wa Bagamoyo, japo wapo katika mazingira yenye mvuto mkubwa wa kujumuishwa na maeneo mengine nchini.

Mji wa Bagamoyo mwaka huu una ugeni mkubwa, unaotokana na historia yake. Thamani ya mji huu ni kubwa hadi umepewa hadhi ya kuwa mwenyeji wa Mkutano Mkuu wa 20 wa Shirika la Ukasisi la Holy Ghost (Wamisionari wa Roho Mtakatifu) la Kanisa Katoliki.

Ugeni huo utajumuisha wajumbe 115 kutoka duniani kote. Hosteli ya Stella Maries mjini
Bagamoyo inaonesha historia ya mji ambapo lilizaliwa Kanisa Katoliki katika Afrika Mashariki mwaka 1868.

Ni heshima kubwa kwetu sisi kama taifa, kuwa mwenyeji wa mkutano mkubwa kiasi hiki na wenye heshima kubwa. Lakini, kwa spidi hii ya kutokuwa na mpangilio mahsusi kuhusu Bagamoyo, mpangilio ambao utalinda hadhi ya mji au la, kwa kuangalia bila kujali makaratasi
yenye mipangilio isiyofanyiwa kazi, Bagamoyo inakufa.