Wapiganaji wa kiisilamu nchini Somalia wanasema kuwa mwanajeshi wa pili wa Ufaransa amefariki kutokana na majeraha yake baada ya jaribio la kumuokoa kukosa kufanikiwa.
Msemaji wa wanamgambo wa al-Shabab ameelezea kuwa komando huyo alifariki kutokana na majeraha ya risasi na kwamba mwili wake na ule wa mwenzake itaonyeshwa baadaye.

Wanamgambo wa Al Shabaab wlaifurushwa mjini Mogadishu kufuatia harakati za jeshi la AU
Ufaransa, ilituma kikosi cha wanajeshi Kusini mwa Somalia siku ya Ijumaa kujaribu kumwokoa jasusi Denis Allex, aliyetekwa nyara tangu mwaka 2009.
Hata hivyo wanamgambo wanasema kuwa yungali hai wakati wakiamua cha kumfanyia.
Msemaji wa Al-Shabab Sheikh Abdiasis Abu Musab, aliambia vyombo vya habari kuwa: ''Komando wa pili alifariki kutokana na majeraha yake. Tutaonyesha miili hiyo kwa Ufaransa''
Siku ya Jumamosi , rais Francois Hollande alisema kuwa wanajeshi hao wawili walitolewa kama kafara katika operesheni hiyo na kwamba bwana Allex aliuawa na wanamgambo waliokuwa wamemteka.

Makabiliano yalianza kati ya al-Shabab na makomando hao baada ya wao kuvamia mji wa Bulo Marer siku ya Ijumaa na Jumamosi.
Waziri wa ulinzi Jean-Yves Le Drian alisema kuwa wanamgambo 17 wa Al Shabaab wameuawa.
Uvamizi ulijiri saa chache baada ya wanajeshi wa Ufaransa kuingilia kati hali nchini Mali.