Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad, akiitikua dua  wazee wa kijiji  chake cha Mtambwe Nyali alipokwenda kuwasalimu Ijamaa. Kulia ni kwake ni mzee Khamis Ali Mohamed na kulia ni bibi Aisha Sheha.
 Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad, akitembea katika katika kijiji chake cha Mtambwe Nyali
 Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad, akitembea katika katika kijiji chake cha Mtambwe Nyali

 Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad, akiwa katika picha ya pamoja na wagombea Ubunge wa jimbo la Chambani kupitia CUF, katika uchaguzi mdogo uliofanyika tarehe 26/06/2013.
Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad, akiongozana na Mbunge wa Chambani, Yussuf Salim Hussein. Picha na Salmin Said, OMKR.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF) Maalim Seif Sharif Hamad, amesema viongozi wa majimbo wanaowakimbia wapiga kura wao hawawatendei haki wananchi waliowachagua.

Amesema ni jambo la kusikitisha kuona baadhi ya wabunge na wawakilishi wakiyakimbia majimbo yao baada ya kuchaguliwa, jambo ambalo linaleta sura mbaya na kutowathamini wananchi.

Maalim Seif ambaye ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar ametoa changamoto hiyo katika Skuli ya Ukutini jimbo la Chambani, kwenye hafla maalum ya kuwapongeza mawakala wa CUF walioshiriki katika uchaguzi mdogo wa Jimbo hilo mwezi Juni, 2013.

Katika hafla hiyo Maalim Seif alimpongeza Mbunge mpya wa Jimbo hilo Yussuf Salim Hussein (CUF), kwa kuanza kuwapa matumaini wananchi wa jimbo hilo, na kumtaka kuendelea na moyo huo wa kuwatumikia wananchi bila ya ubaguzi wowote.

Tangu kuingia madarakani kwa Mbunge huyo miezi mitatu iliyopita, tayari ameshajenga Afisi ya Mbunge pamoja na kuanza matengenezo makubwa ya barabara ndani ya jimbo hilo la Chambani, hali inayowapa matumaini wananchi wa jimbo hilo.

Maalim Seif ametoa wito kwa viongozi wengine wa majimbo kubadilika na kuiga mfano wa Mbunge huyo, ili waweze kutekeleza ahadi za kimaendeleo walizozihidi wakati wa kampeni.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Chambani, Yussuf Salim Hussein, ameipongeza Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kwa kusimamia vyema zoezi la uchaguzi mdogo wa jimbo hilo.

Amebainisha kuwa Tume ya Uchaguzi inaweza kusimamia vyema masuala ya uchaguzi ikiwa itaamua kufanya hivyo, na kuwepo uwezekano wa kufanyika kwa chaguzi huru na za haki katika  visiwa vya Zanzibar.

Mbunge huyo pia amelipongeza jeshi la polisi kwa kuonyesha mfano wa kufanya kazi kidiplomasia, na kwamba utaratibu huo utasaidia kuliweka taifa katika hali ya amani na usalama.

Kabla ya hafla hiyo Maalim Seif aliifungua rasmi Afisi ya Mbunge wa Jimbo la Chambani ambayo itakuwa ikifanya kazi wakati wote kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wa jimbo hilo.